Na Theonestina Juma
UONGOZI wa Kanisa Katoliki Jimbo la Bukoba, umewataka waumini wa kanisa hilo, kulinda kanisa lao alimozikwa masalia ya Mwadhama Laurean Kardinali Rugambwa kwa hali na mali kwa kuzingatia ulinzi shirikishi.
Rai hiyo ilitolewa Oktoba 22, mwaka huu ikiwa ni moja ya matangazo yaliosomwa na mumini wa kanisa hilo aliyejitambulisha kwa mumiliki wa blog hii kwa jina la Bw. Philbert Nshengoma.
"Waumini wote mnatakiwa kulinda jengo la kanisa letu, kwa kuzingatia ulinzi shirikishi, mnapomtilia mtu shaka toeni taarifa mara moja katika kituo cha polisi"alisoma sehemu ya tangazo hilo lilivyosema.
Alisema waumini wa Kanisa hilo, wanatakiwa kuwa macho, kwa kulinda kanisa hilo ambalo limewagharimu mabilioni ya fedha, kwa kuhakikisha linakuwa salama.
Hatua ya kutolewa kwa tangazo hilo kwa maelfu wa kanisa hilo mjini Bukoba, limekuja siku chache baada ya kuibuka kwa migogoro ya kidini na uchomaji moto makanisa ya kikristo kwa fujo hapa nchini.
Jengo la kanisa hilo la Birikira Maria wa Huruma, limefanyiwa upanuzi na ukarabati wa hali ya juu kutokana na fedha za wahisani na waumini wa Jimbo la Bukoba.
Jengo hilo ambalo kwa sasa ndilo linaonekana kuwa la thamani na kivutio kikubwa kwa baadhi ya wageni waozuru mkoani hapa, ndimo alimozikwa kwa mara pili masalia ya Kardianali Rugambwa, hapo Oktoba 6, mwaka huu, baada ya kutaka ifanyike hivyo enzi za uhai wake.
No comments:
Post a Comment