Sunday, September 22, 2013

Uzao wa shule ya sekondari WeruWeru wanogesha sherehe ya kutimiza miaka 50, wamo akina Dkt Asha Migiro na Dkt.Mery Nagu

IMG_0125Waziri Mkuu, Mizengo Pinda akizindua Bwalo la Shule ya Sekondari ya Wasichana ya Weruweru ya Moshi  Vijijini ikiwa na sehemu ya maadhimisho ya miaka 50 ya shule hiyo Septemba 21, 2013. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu) IMG_0143Waziri Mkuu, Mizengo Pinda akipanda  mti kwenye viwanja vya Shule ya Sekondari ya Wasichana ya Weruweru ya Moshi Vijijini  akiwa katika maadhimisho ya miaka 50 ya shule hiyo Septemba  21, 2013.  Wapili kushoto ni mkewe Tunu na Watatu kushoto ni Waziri wa  Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Profesa Anna Tibaijuka na Wapili kulia ni Naibu Waziri  wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, Kassim Majaliwa. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu) IMG_0183Baadhi ya Wanawake waliosoma katika  Shule ya Sekondari ya Wasichana ya Weruweru ya  Moshi Vijijini  wakiimba wimbo wa Shule hiyo katika maadhimisho ya miaka 50  ya shule hiyo   Septemba 21, 2013. (Picha na Ofisi ya waziri
………………..

WAZIRI MKUU Mizengo Pinda amewataka Watanzania kuiga mfano wa shule ya Sekondari ya Weruweru ambao wahitimu wake wa zamani (Alumnae) wameamua kuchangisha fedha na kukarabati shule yao ya zamani.
Ametoa kauli hiyo jana jioni (Jumamosi, Septemba 21, 2013) wakati akizungumza na mamia ya wanajumuiya waliohitimu katika shule hiyo (Alumnae), wanafunzi waliopo pamoja na wageni mbalimbali waliohudhuria sherehe za Jubilei ya miaka 50 ya Shule ya Sekondari ya Wasichana ya Weruweru.
Waziri Mkuu ambaye alikuwa mgeni rasmi katika sherehe hizo alisema: “Watanzania wengi tuna nafasi za kuchangia shule zilizotusomesha. Tuige mfano wa wenzetu wa Weruweru, tukutane na kusaidia shule tulizosoma,” alisema.
Alisema yeye alisoma sekondari ya Pugu kati ya mwaka 1965 na 1967 lakini kumekuwa na juhudi mbalimbali za kuwakutanisha wahitimu wa shule hiyo ambazo hazijawahi kufanikiwa. “Ninawataka mtembee kifua mbele kwa sababu shule yenu imeza yunda zuri sana,” alisema huku akiwasifia wana Weruweru waliohitimu zamani kwa kuamua kuja na wazo hilo jema la kukarabati shule yao ya zamani.
Mapema, akisoma taarifa ya shule hiyo, Mwalimu Mkuu wa Weruweru, Bibi Rosalia Frimini alisema shule hiyo iliyoanzishwa Oktoba 22, 1963 hivi sasa ina wanafunzi 570 wa kidato cha tano na sita tu wanaosoma michepuo ya PCB, EGM,ECA, HGE, HGK na HKL.
Alisema shule hiyo inakabiliwa na changamoto nyingi ikiwemo uchakavu wa maabara, madarasa, mabweni na mifumo ya umeme. Alisema shule hiyo ina upungufu wa watumishi wakiwemo manesi, wapishi, mkutubi na walinzi.
“Shule pia inakabiliwa na tatizo la usafiri.  Landrover 110 iliyopo shuleni ni ya tangu miaka ya 80 na matengenezo yamekuwa makubwa, tunaomba utusaidie kutatua tatizo la usafiri… tunapata shida hasa ikitokea watoto wanaumwa na wanatakiwa kupelekwa hospitali ya mkoa,” alisema.
Akizungumza katika hafla hiyo, Dk. Maria Kamm ambaye aliongoza shule hiyo kwa miaka 22 kuanzia mwaka 1970 hadi 1992, aliiomba Serikali irudishe mfumo wa kidato cha kwanza hadi cha nne kwa shule kongwe ambao ulifutwa na Serikali. Alisema katika kujenga maadili kwa watoto, inabidi waanze tangu wanapoingia sekondari.
“Hawa wa kidato cha tano na cha sita ni wa kupita tu.. umri wa kuumba binti ni kuanzia kidato cha kwanza hadi cha nne. Tunahitaji kuumba mabinti wa Taifa hili kama ambavyo tulikuwa tukifanya huko nyuma,” alisema.
Alisema Sera ya Taifa ya Elimu ya Kujitegemea ilikuwa ndiyo siri kubwa ya kuwaumba wasichana waliopitia shuleni hapo na kwamba ilileta usawa na kuondoa ubaguzi. “Sera hii ilifanya watoto wote wawe sawa, iliondoa ubaguzi shuleni kwa sababu wanafunzi wote walijifunza kazi na kujiamini. Na yote hii ni katika kujenga nidhamu kwa watoto wetu,” alisema.
“Elimu ya Kujitegemea siyo siasa kama wengi wanavyodhani, ni jadi ya mwafrika, ni jadi ya mwanamke. Kujitegemea ndiyo msingi wa maendeleo ya Taifa lolote ulimwenguni, tunaomba Serikali irudishe elimu ya kujitegemea shuleni ili tuwasaidie watoto wetu.”
Naye Naibu Katibu Mkuu Mstaafu wa Umoja wa Mataifa, Dk. Asha-Rose Migiro ambaye ni mhitimu wa shule hiyo alisema Jubilei ya miaka 50 ya Weruweru ni sehemu ya kusherehekea ndoto iliyotimia na ndoto iliyokuwa kweli kwa wanafunzi wengi waliosoma kwenye shule hiyo.
“Shule hii ni ya pekee kwa sababu ilitoa fursa kwa mtoto wa kike pale ambapo hapakuwa na fursa… ilikuwa ni mchanganyiko wa watoto wa viongozi, wafanyakazi na wakulima”.
Akimnukuu Rais wa zamani wa China, Mao tse Tung, aliyesema wananwake wanashikilia nusu ya anga, Dk. Migiro alisema kutokanana usemi huo haiwezekani watu wanaoshikilia nusu ya anga wakaendelea kubaki nyuma.
Alisema shule hiyo imetoa wataalamu mbalimbali wakiwemo wanadiplomasia, wanasiasa, viongozi mbalimbali wa mashirika, taasisi na serikali na pia imetoa rubani wa kwanza mwanamke hapa nchini.
Baadhi wa wanafunzi waliohitimu katika shule hiyo ni Dk. Asha-Rose Migiro, Dk. Mary Nagu, Balozi Mwanaidi Maajar, Bi. Anna Kilango Malecela, Dk. Mwele Malecela, Dk. Hellen Kijo-Bisimba, Hajat Amina Mrisho na wengine wengi ambao wameshika nafasi mbalimbali za uongozi katika mashirika, taasisi na Serikalini.

Operesheni kimbunga awamu ya kwanza yakamilika, sasa ni nyumba kwa nyumba

JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA

WIZARA YA MAMBO YA NDANI YA NCHI
http://www.fullshangweblog.com/wp-content/uploads/2013/09/Kamanda-Sirro-akizungumzia-vurugu-za-wamachinga-Mwanza.jpg

AARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
Operesheni Kimbunga iliyoanza Septemba 6,2013 imemaliza utekelezaji wa Awamu yake ya Kwanza Septemba 20,2013 kwa kutimiza malengo yake kwa mafanikio makubwa.
Hadi kufikia mwisho wa Awamu ya Kwanza wa Operesheni hii, Timu ya Operesheni imefanikiwa kukamata wahalifu wa unyang’anyi wa kutumia silaha pamoja na washirika wao na kuhakiki uraia wa watuhumiwa wa Uhamiaji haramu kwa kutumia maofisa wa Idara ya Uhamiaji kwa kuzingatia Sheria za Uhamiaji. Aidha, suala la Haki za Binaadam limezingatiwa katika Operesheni hii.
Jumla ya Wahamiaji haramu 12,704 wamekamatwa, kati yao Wanyarwanda 3,448 Warundi 6,125, Waganda 2,496, Wakongo 589 Wasomali 44, Yemen 1 na India 1.
Jumla ya Wahamiaji Haramu 194 walirudishwa na kupokelewa nchini baada ya kukataliwa na nchi zao. Watu hao wanasubiri  hatua za kisheria kuchukuliwa kwa kuwa hawana sifa ya kuwa Raia wa Tanzania na pia wamekosa sifa ya kuwa raia wa nchi jirani ambapo Serikali iliwapeleka baada ya vigezo vya kuthibitisha kuwa ni raia wa nchi hizo kukamilika.
Wakati Operesheni kimbunga inafanyika katika Awamu yake ya Kwanza kuanzia Septemba 6, 2013, jumla ya wahamiaji haramu 2,129 walikubali kuondoka nchini kwa hiari yao na Wahamiaji Haramu  8,696 waliondoshwa nchini kwa amri ya Mahakama baada ya kupewa hati ya kufukuzwa nchini. Watuhumiwa wa Uhamiaji Haramu 1,852 waliachiwa huru baada ya Serikali kuthibitisha uraia wao wakati wengine 2,286 wanaendelea na mahojiano ili kuthibitisha uraia wao. 
Operesheni Kimbunga pamoja na kushughulikia wahamiaji Haramu ilifanikiwa kukamata jumla ya Watuhumiwa 212 wa unyang’anyi wa kutumia silaha na Majangili wa Tanzania 23. Mabomu 10 ya kutupwa kwa mkono, bunduki/silaha 61 zikiwemo bunduki aina ya SMG 5, Shot Gun 8, Mark IV 1, Riffle 1, Pistol 1, Pisto za kienyeji 3 na Magobole 42 pamoja na mitambo Miwili 2 ya kutengeneza silaha aina ya Magobole.
Risasi 665 zilikamatwa zikiwemo za bunduki aina ya SMG na SAR risasi 561, Shot Gun risasi 22, Gobole risasi 82 na Fataki 8, Suruali Sare za Jeshi na Kibuyu cha Maji vya Jeshi la Wananchi wa Tanzania.
Jumla ya Ng’ombe 8,226 walikamatwa wakiwa wanachungwa katika maeneo ya Tanzania hususan katika hifadhi za misitu. Pia kiasi cha Tsh. 32,510,000/= zimepatikana ikiwa ni tozo za faini ya ng’ombe walioachwa kwenye hifadhi ya Taifa.
Ngozi za wanyama aina ya Duma(1), Swala (2), Nyati (1) na vipande 10 vya Nyama vinavyodhaniwa kuwa Nyara za Serikal, Vipande viwili vya meno ya Tembo pamoja na Mbao 2,105, Magogo 86, Mkaa Magunia 467,Gongo Lita 375, Mtambo wa Gongo mmoja (1), Bangi Kilo 77 na Makokoro yanayotumika kuvuna Samaki kinyume cha sheria  vilikamatwa katika kipindi cha Wiki Mbili za Awamu ya Kwanza ya Operesheni Kimbunga.
Takwimu zinaonyesa kuwa Mkoa wa Kagera unaongoza kwa kukamata wahamiaji haramu 7,001 ukifuatiwa na Mkoa wa Kigoma ambaPo wahamiaji haramu 5,005 walikamatwa wakati mkoa wa Geita wamekatwa Wahamiaji Haramu 698.
Changamoto
Pamoja na mafanikio yaliyopatikana kumekuwepo na changamoto zilizojitokeza ikiwa ni pamoja na hali ya maisha mchanganyiko ya Watanzania asilimia 60% na Wahamiaji asilimia 40% katika mikoa ya mpakani hii ni kwa mujibu wa tafiti mbali mbali za masuala ya kiuhamiaji zilizowahi kufanyika katika mikoa hiyo.
Changamoto nyingine ni baadhi ya wananchi wenye nia mbaya au kulipizana visasi walitaka kutumia zoezi hili kuweza kukomoana kwa kuwataja baadhi ya watu kuwa ni wahalifu kumbe ni uongo na baadhi ya wahamiaji baada ya kukamatwa walikosa sifa za uraia wa Tanzania na hata waliporudishwa kwenye nchi wanazodhaniwa kutoka walikosa sifa za uraia na kuleta mgongano kuhusiana na uraia wao yaani kwa kiingereza (Stateless citizenship) .
Changamoto nyingine zilizojitokeza ni pamoja na ukosefu wa Vitambulisho vya Uraia (Utaifa) ambako kulileta tatizo katika kuwatambua Wahamiaji Haramu na kutokuwepo kwa uzio wa kuzuia mipaka ya nchi yetu hivyo Wahamiaji Haramu wanapopelekwa kwao wanarudi kupitia vipenyo visivyo halali yaani njia za panya.
Sheria ya Maliasili na Utalii (The Forest Act & Wild Life Conservation Act) kutoendana na hali halisi ya uhalifu wa uhujumu wa Maliasilia, mfano kifungu cha 81 (2) kinatoa adhabu ya faini kuanzia shilingi Elfu Thelathini (30,000/=) hadi Milioni Moja na uzoefu unaonyesha kwamba wanaotenda makosa hayo hupigwa faini chini ya Shilingi Laki Tano (500,000/=) bila kujali thamani ya mali aliyokamatwa nayo, isipokuwa maamuzi hutegemea utashi wa Mahakama.
Matarajio
Baada ya kukamilisha Awamu ya Kwanza ya Operesheni Kimbunga tunatarajia Serikali kushughulikia changamoto zilizojitokeza ili kupunguza baadhi ya matatizo katika mikoa ya Kagera, Kigoma na Geita hususan yanayohusia na uhalifu na masuala ya kiuhamiaji.
Tunatarajia kuanzisha kikosi kazi kila mkoa kwa ajili ya kufanya ufuatiliaji wa wahalifu sugu wanaotumia silaha za kivita na wale wanaowafadhili.
Aidha, uhamasishaji utafanyika kuanzia ngazi ya familia, Kitongoji, Mtaa/Kijiji, Kata/Shehia, Tarafa, Wilaya Mkoa na Taifa kuhamsisha jamii kuimarisha misingi ya ulinzi na usalama kupitia kwenye kamati zilizopo na kutoa taarifa mara moja pindi panapojitokeza jambo lolote linalohusu ulinzi na usalama katika maeneo yao.
Aidha, tunatarajia kujipanga kimkakati ili kuona namna ya kushughulikia baadhi ya Wahamiaji Haramu waliokosa sifa za uraia na kurudishwa nchini mwao ambao bado wanang’ang’ania kwa kusema wao ni Watanzania (stateless citizenship).
Washiriki                                                                                                                                      
Operesheni Kimbunga ilishirikisha Vyombo Vya Ulinzi na Usalama wakiwemo Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ), Polisi, Usalama wa Taifa, Uhamiaji, Magereza, TAKUKURU, Taasisi nyingine za Serikali zikiwemo Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na  Idara za Mifugo,  Ardhi, Kilimo, Uvuvi, Misitu, Afya na Idara ya Wanyama Pori.
Hitimisho
Opereshi Kimbunga ilifanyika kwa kufuata Sheria, Kanuni na Taratibu za nchi. Aidha, suala la Haki za Binaadam lilizingatiwa na hadi sasa hakuna malalamiko yeyote yaliyopokelewa.
 Hata hivyo, juhudi na nguvu zaidi zitaelekezwa katika kukamata Majambazi, Silaha Haramu, Majangili na Wahamiaji Haramu. 
Mafanikio yaliyofikiwa yametokana na ushirikiano wa Maofisa Wakuu Waandamizi, Maofisa wa Kati, Wakaguzi na Askari wote wa vyeo mbali mbali walioshiriki kwenye utekelezaji wa operesheni hii. Kila mtendaji alitimiza wajibu na majukumu yake na ndiyo maana malengo ya utekelezaji wa operesheni hii yamefikwa kwa kiasi kikubwa. Hata hivyo huu ni mwisho wa Awamu ya Kwanza ya operesheni na mwanzo wa Awamu ya Pili ya Operesheni Kimbunga kwa maana nyingine Operesheni inaendelea mpaka hapo hali ya usalama ya mikoa hii Mitatu itakapokuwa shwari.
 Taarifa hii imetolewa na:
Naibu Kamishna wa Polisi Simon Sirro kwa niaba ya Kamanda wa Operesheni Kimbunga Mwanza, Septemba22,2013

Happiness Mrembo Dodoma ndiye Miss Tanzania 2013/2014

1Redd’s miss Tanzania 2013 mrembo Happiness Enock Watimanywa toka mkoani Dodoma akiwa na washindi wenzake wa shindano la Redd’s miss Tanzania mara baada ya kutangazwa kuwa mshindi kwenye shindano lililofanyika kwenye ukumbi wa Mlimani Cituy jijini  Dar Es Salaam,Kulia ni mshindi wa Pili Latifa Mohamed toka kanda ya Temeke na kushoto ni mshindi wa tatu Clara Bayo toka kanda ya Temeke 2Mkurugenzi wa masoko wa Tbl Kushilla Thomas akimkabidhi funguo za gari mshindi wa shindano la Red’s miss Tanzania 2013 mrembo Happiness Enock Watimanywa toka mkoani Dodoma  mara baaada ya kunyakua tajio hilo na kuwashinda washiriki wenzake 29  toka mikoa mbalimbali ambapo pamoja na gari lakini pia amepata kiasi cha shilingi milioni nane

Siku ya tembo yazinduliwa

 Gari la Maliasili likiwa limebeba Meno ya Tembo, wakati wa kujiandaa na Maandamano kuelekea Mlimani city kwa ajili ya maadhimisho hayo
 Msanii wa Muziki wa Kitanzania Mrisho Mpoto akianza kuongoza maandamano kutoka Chuo kikuu cha Dar es salaam Kuelekea Ukumbi wa Mlimani City leo.
 Maandamano ya Siku ya Tembo yakiwa yanaendelea kuelekea ukumbi wa Mlimani City kwa ajili ya Kongamano hilo
 Wasanii wa Mrisho Mpoto wakiwa wamebeba chatu katika maadhimisho ya Siku ya Tembo Kitaifa leo
Mkurugenzi wa wanyamapori  Wizara ya maliasili na utalii Prof. Alexander Songorwa akisoma Hotuba kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na utalii.
 Wadau mbalimbali wa utalii na kupinga mauaji dhidi ya Tembo wakiwa wanafuatilia kwa umakini maadhimisho ya Siku ya Tembo kitaifa.
 Wanafunzi kutoka Shule ya Jitegemee wakiwa wanafuatilia kwa umakini Maadhimisho hayo
Mrisho Mpoto akiwa anatumbuiza katika Maadhimisho hayo ya siku ya Tembo
Mmoja ya waratibu wa Shuguli za Siku ya Tembo kitaifa Issa Isihaka kushoto akifuatilia kwa umakini siku ya Tembo kitaifa
Picha ya Pamoja ya Viongozi Mbalimbali wa Serikali na wadau

Wednesday, September 18, 2013

Tanzania, Rwanda na Burundi zasaini mkataba kuzalisha umeme Mto Rusumo



Na Theonestina Juma, Bukoba
TANZANIA, Rwanda na Burundi zimesaini mkataba wa makubaliano ya awali ya kuanza utekelezaji wa mradi wa kufufua umeme katika maporomoko ya mto Rusumo  ya megawati 80.
Mkataba wa makubaliano hayo yamesainiwa  jana (leo) katika Manispaa ya Bukoba ambapo ulihudhuriwa na  wajumbe  mbali mbali kutoka nchi zote tatu.
Akifungua mkutano wa kusaini makubaliano  ya mradi huo, Waziri wa Nishati na Madini nchini, profesa Sospeter Muhongo alisema hatua hiyo inafungua mlango wa kuanza utekelezaji wa mradi huo.
Alisema mradi huo unatarajiwa kuanza mwaka 2015 hadi 2018 ambapo utakuwa takribani miaka minne hadi kukamilika kwake.
Alisema katika utekelezaji wa mradi huo umegawanyika katika sehemu mbili ambapo sehemu ya kwanza wataanza kufufua nishati hiyo, ambayo itagharimu  dola milioni 340 kwa pande za nchi zote tatu na itafadhiliwa na Benki ya Dunia  baada ya kuonesha nia.
Halikadhalika sehemu nyingine ni ujenzi wa njia ya kusafirishia nishati hiyo kutoka mto Rusumo hadi Nyakanazi  katika njia ya kwenda nchi jirani ya Burundi, itakagharimu dola milioni 130.
Alisema kati ya hizo fedha ndizo zitajumuisha masuala ya kufidia watu ambao watatakiwa kuondoka katika maeneo yao kupisha utekezaji wa mradi huo, ambapo  Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB)imeshaonesha nia ya kutoa  dola milioni 95.
Halikadhalika kati ya dola hizo milioni 130 benki zingine nazo zimekubali katika kuwasaidia, ambapo alizitaja benki hizo kuwa ni pamoja na Beenki ya misaada ya ujerumani ( KFW), benki ya ujasiliamali ya ujerumani na benki ya Uholanzi.
Profesa Muhongo alisema pindi mradi huo utakapokamilika  utaweza kuzalisha umeme megawati 80 ambapo kila nchi itapata mgawao sawa ambao ni megawati 27.
Hata hivyo,Waziri Muhongo alitoa tahadhari kwa pande zote za nchi hizo tatu kuwa makini katika harakati za utekelezaji wa mradi huo, kwa kuondoa ukiritimba unaoweza kujitokeza na kusababisha kuvunjika kama ilivyotokea kwa Jumuiya ya Afrika Mashariki mwaka 1977.
“Katika harakati za utekelezaji wa mradi huu, lazima nchi zote kuwa makini, kuondoa ukiritimba unaoweza kujitokeza ya mtu kuajiri ndugu zake… hasa masuala ya rushwa…,tunahitaji umeme kwa ajili ya maendeleo ya wananchi”alisema.
Alisema iwapo mradi huo utakamilika nchi zote tatu zitaweza kuwa na nishati hiyo ya kutosha na hata kuanza kujenga mtandao kwa nchi jirani kwa lengo la kuwauzia.
Alisema hadi kufika mwaka 2015 Tanzania itakuwa na megawati ya umeme 3,000 ambapo kwa sasa  nchi unao megawati 1,501.2.
Naye Waziri wa Miundombinu kutoka nchini Rwanda, Profesa Silas Rwakabamba akizungumza katika mkutano huo, kabla na baada ya kusaini mktaba wa makubaliano hayo, alisema mradi huo utakapokamilika utawezesha wananchi kupata umeme wa kutosha na hivyo kuwa kichocheo cha ukuwaji wa uchumi katika nchi hiyo.
“Mimi ni shahidi katika makubaliano haya kwa nchi yangu, tunaamini nishati ya umeme ni muhimu katika ukuaji wa uchumi na maendeleo ya wananchi”alisema.
Mradi wa kufufua umeme katika  maporomko ya mto Rusumo  kupendezwa kuanza  tangu mwaka 1974 , ambapo hata hivyo utekelezaji wake haukuweza kuendelea hadi mwaka 2005 upembuzi yakinifu ulipoanza na kwa sasa utekelezaji wake unaanza.
Mawaziri waliohudhuria katika mkutano huo ni pamoja na Profesa Sospeter Muhongo kutoka Tanzania, Waziri wa Miundombinu, Profesa Silas Rwakabamba  wa Rwanda na  Waziri wa nishati na Madini, Bw. Manirakiza C'ome kutoka nchini  Burundi na Naibu Kamishna wa nishati ya masuala ya umeme nchini, Mhandisi Innocent Luoga.
 Pia wawakilishi kutoka benki ya Maendeleo ya  Afrika, Bi. Stella Mandago na wa Benki ya Dunia, Bw. Paul Baringanire.

Mradi wa kuzalisha umeme kwa kutumia maporomoko ya mto Rusumo kwa nchi tatu waiva, mkataba wake wa awali wasainiwa Bukoba

 Mawaziri wa nchi tatu wa kwanza kulia  waziri wa Miundombinu wa rwanda Silas Rwakabamba, waziri wa Nishati na madini wa Tanzania Sospeter Muhongo na Waziri wa  Nishati wa Burundi Manirakiza C'ome wakiwa katika  picha ya pamoja katika viwanja vya  ukumbi wa Bukoba hotel E.L.C.T.
                                       mkutano wa kuwekeana mkataba umefanyika bukoba hotel
                         Sehemu ya waliokaa baadhi ya  wajumbe kutoka katika nchi za Tanzania, Burundi na Rwanda waliohudhuria katika kikao hicho cha kutiliana mkataba wa makubaliano ya kufufua mradi wa umeme katika maporomoko ya mto Rusumo.
Add caption
       Mawaziri kutoka nchi tatu wakiwa makini kusikiliza maelekezo yaliokuwa yakitolewa ukumbini hapo.                                              
 Bw. Paul Baringanire mwakilishi wa Benki ya Dunia ambao wamekubali kutoa dola mlioni 340 kwa ajili ya kufufua  mradi huo.
 Bi Stella Mandago mwakilishi wa benki ya maendeleo ya Afrika ambao nao wameonesha nia ya kutoa dola milioni 130.
 Waziri wa Burundi Bw. Manirakiza C'ome ambaye alikuwa akiongea kwa kifaransa na kutafsiriwa na mkalimani akieleza namna walivyojipanga katika  utekelezaji wa mradi.
 Waziri wa  miundo mbinu wa nchini Rwanda Profesa Silas Rwakabamba akieleza mikakati ya nchi yake katika utekelezaji wa mradi.
 Waziri wa Nishati na Madini wa Tanzania Profesa Sospeter Muhongo akifungua mkutano huo wa kutiliana mkataba wa makubaliano ya kufufua umeme kutokana na maji ya maporomoko ya mto Rusumo.
 
                       Mawaziri wa nchi tatu wakiwa katika picha ya pamoja na wafadhili wa mradi huo.
      Picha ya pamoja  ya Mawaziri, Wafadhili na baadhi ya wajumbe kutoka nchi tatu.

        Waziri wa Nishati na Madini wa Tanzania Profesa Muhongo akisaini mkataba wa awali wa makubaliano.
      Mawaziri  kutoka nchi tatu wakiwa wameshikilia mikataba baada ya kusaini.
          Waziri wa  Miundombinu wa nchini Rwanda profesa Rwakabamba akisaini mkataba
Mawaziri hao wakiwa katika picha ya pamoja na wajumbe wa bodi waliosimama nyuma yao kutoka nchi zote tatu.

Monday, September 16, 2013

Mnyarwanda mwingine ajinyonga ni katika Operesheni kimbunga, kisa hakutaka kurudi kwao

Na Theonestina Juma, Kagera,

RAIA mwingine wa Rwanda, Bw.Michael John (70) amejinyonga kwa kutumia shuka lake chumbani kwake Wilayani Missenyi,akihofia kurejeshwa nchini Rwanda na Operesheni kimbunga inayoendelea.

Akizungumza na gazeti hili Mtendaji wa kijiji cha Lwano, Bw.Deusdedith NjunwaMulokozi alisema tukio hilo limetokea usiku wa kuamukia  leo Septemba 16,mwaka huu, katika kitongoji cha Chaibumba kijiji cha Lwano kata ya Ishozi Tarafa  ya Kiziba Wilayani Missenyi.

Alisema Bw.John  alikutwa na mkewe Bi.Rahel Kagawa (66), mwili wake ukiwa unaning’inia juu ya dari akiwa tayari ameshakata roho saa 1.07 asubuhi baada ya usiku kukorofishana na mumewe huyo na kuamua kwenda kulala kwa jirani.

Alisema chanzo cha Bw. John kujinyonga ni baada ya kupata taarifa kuwa wahamiaji haramu wote wanarejeshwa nchini mwao, ambapo toka siku hiyo alikuwa akisema kuwa hawezi kurudi Rwanda na badala yake atajiua.

“Chanzo cha Bw. John kujiua ni kuhofia kurejeshwa nchini mwake Rwanda, ambapo alikuwa akikataa kurudi huko kwa madai kuwa alitoka huko akiwa kijana na hawezi kurejea tena nchini humo”alisema mtendaji huyo.

Alisema Bw. John  aliingia  kijijini hapo tangu mwaka 1983 hadi leo hadi mauti yanamkuta, ambapo alioa mwanamke wa Kitanzania  Bi. Rahel ambaye ni mzaliwa wa kijiji cha Ishozi  na kuishi naye kwa kipindi cha miaka 30 na hawakufanikiwa kupata mtoto.

Alisema kabla ya kuchukua hatua hiyo, Bw. John alikuwa akikorofishana na mkewe  na kukimbia kwenda kulala kwa majirani kutokana na ulevi na kurudi kesho yake asubuhi na kumkuta akiwa katika hali nzuri.

“Kwa siku ya jana mkewe aliamua kukimbia na kwenda kulala kwa majirani kama ilivyo kwa wanadoa wanapokorofishana na alirejea asubuhi ili kuweza kuangalia kama hali imetulia kutokana na ulevi, lakini matokeo yake amemkutaka akiwa ameshajinyonga”alisema.

Alisema  Bi. Rahel aliporejea nyumbani alikuta mlango ukiwa umefungwa ambapo si kawaida yake,  alilazimika kutumia nguvu kufungua mlango huo na kukuta mumewe akiwa amejinyonga.

Alisema wanandoa hao walikuwa wakiishi maisha ya kawaida tu na walikuwa wakijishughulisha na kazi ya kilimo pekee.

Mtendaji huyo ametoa wito kwa wahamiaji haramu walioko katika kijiji hicho kuacha tabia ya kujiua kwani sio jibu na badala yake  wafuate sheria na utaratibu unaotakiwa na serikali kama wanapenda kuishi nchini.
Hili ni tukio la pili la wahamiaji  haramu kujingonga, baada ya, Bw. Francis Mathias (75),mkazi wa kitongoji Kikukuru kata Kikukuru, tarafa Mabira wilayani kujinyonga Septemba 9, mwaka huu baada ya mkewe kugoma kuuzwa mali zote ili warejee nchini Rwanda

Walimu Wakuu wawili wa shule za sekondari mkoani Kagera wafa katika ajali Biharamulo, walikuwa wakienda kwenye semina elekezi ya kuboresha elimu mkoani Kagera



Na Theonestina  Juma, Bukoba

WALIMU Wakuu wawili wa shule za sekondari  katika halmashauri ya wilaya ya Bukoba mkoani Kagera,wamefariki dunia papo hapo huku wengine saba wakijeruhiwa vibaya katika ajali ya barabarani wakati wakienda katika semina elekezi ya kuboresha sekta ya elimu mkoani hapa inayofanyika Wilayani Ngara.

Kwa mujibu wa habari kutoka eneo la tukio, ajali hiyo imetokea Septemba 15, mwaka huu majira ya jana jioni Wilayani Biharamulo wakati wakiwa safarini kulekea wilayani Ngara baada ya kusaidiwa usafiri na Afisa vifaa na takwimu kutoka ofisi ya Mkuu wa Mkoa Kagera Bw. Johanes Katanga ambaye alikuwa dereva wa gari hilo, naye pia amejeruhiwa.

Chanzo cha ajali hiyo imeelezwa kuwa dereva wa gari hilo aina  Noah  ambalo namba yake ya usajili halijajulikana alikuwa akijaribu kumkwepa mwendesha baiskeli ambapo gari hilo lilipasuka matairi yote ya mbele na kupinduka.

Wakuu hao wa Shule za sekondari waliofariki ni pamoja na Bi. Agness Philipo wa shule ya sekondari ya Bunjunangoma na  Bw.Makoye Bloho wa shule ya sekondari ya Tunamkumbuka shule hizo zote ziko katika halmashauri ya  wilaya ya Bukoba.

Kwa mujibu wa Katibu wa Wakuu wa shule za sekondari Mkoani Kagera, Bw. Emmanuel Muganyizi, Bi.Philipo alifariki  dunia papo hapo baada ya kupata jeraha kubwa sehemu ya kichwani.

Aidha Bw.Bloho amefariki dunia leo njia wakiwa wamefika wilayani Sengerema wakati wakikimbizwa katika hospitali ya Rufaa ya Bugando kwa matibabu zaidi.

Alisema Bw.Brongo alifia njia wakati wakisafishwa pamoja na mwalimu mwenzake Bw. Themistocles Rwabangira  wakati wakipelekwa katika hospitali ya Rufaa ya Bugando  Jijini Mwanza baada ya wao kuonekana kuumia zaidi.

Hata hivyo, mwalimu Rwabangira  amefikishwa hospitalini hapo ambapo vipimo vimebaini kuwa amevunjika mbavu na mikono na mwili wa Bw. Bloho umehifadhiwa katika hospitali ya Rufaa ya Bugando..

Aliwaja walimu waliojeruhiwa katika ajali hiyo kuwa ni pamoja na Bw. Shafii wa shule ya sekondari ya Ruhunga na Bw.Philbert Ferdinand wa Karagabaine.

Wengine ni pamoja na  Bi.Pelagia Thadeo, Bw. Malimbo wa shule ya sekondari ya Kalema na Bw. Katanga Afisa vifaa na Takwimu Mkoa Kagera ambaye alikuwa dereva wa gari hilo na mumiliki wake ambaye aliwasaidia usafiri walimu hao, wote wamelazwa katika hospitali teule ya Biharamulo.

Alisema Bi.Philipo anatarajiwa kuzikwa kesho Kemondo Bukoba vijijini na Bw.Bloho atazikwa nyumbani kwake Wilayani Magu jijini Mwanza.

Alisema kutokana na majonzi hayo kikao kilichotakiwa kianze leo kimeahirishwa hadi kesho.

Semina hiyo inawashirikisha walimu Wakuu wa shule za sekondari za umma kutoka wilaya zote za mkoa Kagera.