Monday, October 13, 2014

Haya ndiyo urithi wa Lady Jay Dee




Hili ni gari kwa ajili ya Bend yake inayojulikana kama Machozi Band






Hii ndo nyumba anayoishi mwanadada Lady Jay dee 




Hii ndo gari anayomiliki aina ni Super Murano 





Hu undo mgawa anaomiliki mwanadada lady Jay dee unaojulikana kama Nyumbani lounge 



Jide anajivunia kushinda Tuzo za Tanzania, Kilimanjaro Music (2004) kupitia kipengele cha Albamu Bora ya R&B (Binti), mwaka 2006 kupitia Tuzo za Pearl of Africa Music alizoshinda kama Mwanamuziki Bora wa Kike kutoka Tanzania

.Kama hiyo haitoshi, mwaka 2007, Jide alishinda Wimbo Bora wa kushirikiana (Hawajui) kupitia Tanzania Music Awards alioshirikiana na MwanaFA.

 Mwaka 2008, kupitia Tanzania Music Awards, Lady Jaydee alishinda Tuzo ya Mwanamuziki Bora wa Kike pamoja na za Pearl of Africa Music katika kipengele hichohicho, Kisima Music Awards (Wimbo Bora wa Mwaka) uitwao Anita alioshirikiana na Matonya.

Mwaka 2009, alishinda Tuzo za Tanzania Music (Wimbo Bora wa Mwaka), Anita kisha 2010 Tanzania Music Awards (Mwanamuziki Bora wa Kike), mwaka 2011 Mwanamuziki Bora wa Kike na Wimbo Bora wa Afrika (Nitafanya, aliomshirikisha Kidum kutoka Kenya na mwaka jana (Mwanamuziki Bora wa Kike).

Kwenye suala la kujitanua kibiashara ndiyo ilisababisha mwaka 2010 afikie makubaliano na Kampuni ya Mohamed Enterprises kuzalisha maji yenye nembo ya jina lake ingawa biashara hiyo haikudumu kwa muda mrefu. 

Hakukata tamaa, cheche zake kwenye ujasiriamali zilizaa matunda kwenye mgahawa wake wa Nyumbani Lounge uliopo Ada Estate, Kinondoni, jijini Dar ambao unamuingizia mkwanja hadi sasa.

Heshima kwake ilizidi kuongezeka, taratibu alifanikiwa kujijenga katika maisha yake binafsi kama ujenzi wa nyumba yake ya kifahari iliyopo Kimara, Dar.

 Mali kama magari ya kutembelea, magari ya kazi zake za muziki havimpigi chenga.

Katika kuonesha muziki na ujasiriamali kwake vimevuka mipaka, ilifika wakati walishauriana na mumewe aachane na kazi ya utangazaji kwa muda ili aweze kusimamia miradi yao ambayo ilihitaji kutanuka zaidi jambo ambalo limefanikiwa.

Wakamatwa shambani wakilima wakiwa uchi kama walivyozaliwa

POLISI mkoani Simiyu inawashikilia watu wanne wa familia moja kwa tuhuma za kukutwa wakilima katika shamba la familia yao, huku wakiwa watupu kama walivyozaliwa.

Kaimu Kamanda wa Polisi mkoani Simiyu, Venance Kimario alisema ofisini kwake jana kuwa wanafamilia hao wamekamatwa wakihusishwa kushiriki katika imani za kishirikina.

Alisema polisi walipata taarifa za siri kutoka kwa raia wema kuhusu wanafamilia hao, kulima shamba huku wakiwa watupu na kuamua kufuatilia, na walipofika eneo la tukio saa 12 za asubuhi, walikuta wanafamilia hao wakilima huku wakiwa uchi wa mnyama.

Alitaja waliokamatwa kuwa ni baba wa familia hiyo, Makoye Gamoge (42) na mke wake Neema Kigela (31), watoto wao wawili (majina yamehifadhiwa).

Kamanda Kimario alidai familia hiyo inatuhumiwa kwamba wamekuwa wakilima huku wakiwa uchi, kutokana na imani za kishirikina kuwa kwa kufanya hivyo, wataongeza tija na mazao yataongezeka maradufu na hivyo kuwakwamua kiuchumi.

“Kwa mujibu wa maelezo yaliyotolewa na baba wa familia hiyo kwenye kituo cha Polisi, kulima kwa mtindo huo kunalenga kuleta mabadiliko makubwa katika sekta ya kilimo cha jembe la mkono,” alisema Kamanda Kimario.

Makoye anadaiwa kusema mbinu hiyo mpya na ya aina yake ni sehemu ya utekelezaji wa maelekezo ya ndugu yao ambaye ni mganga wa jadi, aliyefariki mwaka jana kwa maradhi ambayo hata hivyo hawayafahamu.

Kwa sasa watuhumiwa hao wanashikiliwa Polisi na baada ya uchunguzi kukamilika, watafikishwa mahakamani kujibu mashitaka 

Saturday, October 11, 2014

SHIWATA yandaa misa maalum ya Kumkumbuka Baba wa Taifa Kambarage Nyerere

Baba wa Taifa, Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere enzi za uhai wake
Na Mwandishi Wetu
MTANDAO wa Wasanii Tanzania (SHIWATA) umeandaa ibada maalum ya kumkumbuka Baba wa taifa, Hayati Mwalimu Julius Nyerere itakayofanyika katika mashamba yao yaliyopo kijiji cha Ngarambe, Mkuramga mkoa wa Pawani.
Mwenyekiti wa SHIWATA, Cassim Taalib alisema jana kuwa katika ibada hiyo itaongozwa na Shekhe wa Mkoa wa Dar es Salaam, Alhad Musa Salum kwa upande wa Waislam na Padri John Solomon kwa upande wa Wakristo.
Taalib alisema katika ibada hiyo Mkuu wa Wilaya ya Mkuranga, Mercy Silla na Mkurugenzi wa Halmashauri hiyo wamealikwa kuhudhuria ambayo itakuwa sambamba na ugawaji wa mashamba kwa wanachama ambao wamekubali kulima katika shamba la SHIWATA lenye ekari 500.
Alisema SHIWATAitaendelea kuenzi fikra za Hayati Mwalimu Nyerere alizowahi kuzifanya na kuziendeleza wakati wa uhai wake ambako wasanii waliitikia mwito kwa kuanzisha kijiji chao cha Mwanzega chenye ukubwawa hekari 300 za makazi ambako mpaka sasa zimejengwa nyumba 66 na nyingine zinajengwa na kukabidhiwa Desemba mwaka huu.
Alisema SHIWATA yenye wanachama zaidi ya 8,000 imekuwa ikihamasisha wanachama wakewajenge nyumba katika kijiji chao ambacho Serikali imekitambua rasmikwa kukizindua kupitia Mbio za Mwenge wa Uhuru Julai mwaka huu.
Ofisa Habari wa SHIWATA

Abiria 381 waliokuwa wakisafiri na Mv. Victoria waingiwa na taharuki,baada ya meli kuzimika ghafla ziwani


Na Theonestina Juma, Kemondo Bay
ABIRIA 381 waliokuwa wakisafiri na Meli ya Mv. Victoria  kutoka Bukoba  kuelekea Jijini Mwanza wameingia na taharuki kubwa baada ya meli hiyo kuzimika ghafla ziwani. 
Katika tukio hilo abiria hao inadaiwa kuwa walianza kunyanyang'anya maboya huku kukiwa hakuna hata mfanyakazi mmoja melini aliyejitokeza kuwatangazia wachukue tahadhari gani wala kuwatuliza.
Kutokana na hali hiyo, nahodha wa meli hiyo alijitahidi kuikokota meli hiyo hadi bandari ndogo ya Kemondo ambapo abiria wote walilazimika kulala hapo bila kujua hatima yao.
 Meli hiyo ilizimika usiku wa kuamukia Oktoba 11 mwaka huu saa 6:00 usiku ambapo si kawaida meli hiyo kuwasili katika bandari ya Kemondo kwa muda huo.
 Kwa mujibu wa baadhi ya abiria waliokuwa wakisafiri na meli hiyo waliondoka bandari ya Bukoba majira 3.00 usiku kama ilivyo kawaida ya meli hiyo na kufika kemondo saa 6:00 badala ya saa 4:30 hadi saa 5:00.
 Bw.Gervas Mugisha, alisema  wakati wanaondoka bandari ya Bukoba  baada ya mwendo wa saa moja waliona Meli ikianza kupoteza mwelekeo muda mfupi baadaye ilizimika na  tena kuanza safari bila kutangaziwa kitu chochote na watumishi wa meli hiyo.
 Alisema"tukiwa bado hatujafika Kemondo Meli ilizimika mara tatu hali hiyo iliwatia hofu abiria na kuanza kukimbilia maboya na kunyang’anyana hadi kufikia hatua ya kuyachana ili kila mtu akose"
 Hata hivyo kutokana na hali hiyo walilala bandari yake mondo bila kupewa maelekezo yoyote kulipopambazuka wananchi waliokuwa safarini waliamua kujimwaga katika barabara kuu iendayo Mwanza wakishinikiza uongozi wa meli hiyo kuwarejeshea nali zao.
 Nahodha wa meli hiyo, Bw.Bembere Samson alisema tatizo lililotokea ni kufeli kwa mfumo wa umeme na kusababisha kupoteza mweleko kwa muda wa dakika10.
 Bw.Samson, alisema tatizo la mfumo wa meli hiyo haihitaji matengenezo makubwa bali inahitaji kubadilisha kifaa ambacho kilitarajiwa kuletwa na ndege kutoka jijini Mwanza.
Hata hivyo alisema kuwa, kuchelewa kufika kwa meli kwa wakati unategemeana uzito wa mizigo uliobebwa ndani ya meli na sio ubovu.
 Alisema, meli hiyo inauwezo wakubeba abiria 1200 lakini jana ilikuwa na abiria 381 na inauwezo wakubeba tani 200 za mizigo bila kubainisha kwa jana walikuwa wamebeba tani ngapi za mizigo.
Naye Afisa Mfawidhi wa Mamalaka ya Uthibiti wa Usafirishaji wa Majini na nchi Kavu  (SUMATRA ) Kapteni Alex Katama, alisema meli hiyo haina hitilafu yoyote lakini tatizo lililojitokeza ni la kawaida tu.
"Meli hiyo iko salama tatizo lililotokea ni la kawaida sio ajabu mfumo wa umeme ndio ulioleta hitilafu"alisema.
 Alisema kulingana na utaratibu na kanuni za sumatara chombo chochote kinacho tumia Injini mbili hakiwezi kuruhusiwa  kuendelea na safari kwa kutumia Injini moja.
 Alisema, meli hiyo ya Mv Victoria ina mfumo wa kisasa wa kuongoza meli kwa kutumia umeme, waliotoka Bukoba kwa kutumia mfumo mbadala na ndio maana walilazimika kutia nanga katika bandari ya Kemondo kwa usalama wa Abiria.
 Hata hivyo baadaye meli hiyo ilitengemeaa na abiria kuendelea na safari zao kuelekea Jijini Mwanza.

Friday, October 10, 2014

Mwalimu wa shule ya sekondari Kagemu avamiwa kanisa usiku wa manane auawa kwa mapanga


Na Theonestina Juma, Bukoba

WATU wasiojulikana wamevamia Kanisa usiku wa manane na kumuua kikatili  mwalimu wa shule ya sekondari ya Kagemu kwa kumcharanga mapanga hadi kufa huku mtu mwingine akikatwa mguu wa kushoto.

Mauaji hayo ya kikatili yamefanyika ndani ya kanisa  la Pentekoste Assemblies of God ( PAG ) iliko katika Kata ya Kitengaguro usiku wa manane mwalimu huyo pamoja na wenzake wakiwa kwenye mkesha wa maombi kanisani humo.

Mwalimu aliyeuawa kikatili kiasi hicho amejulikana kuwa ni Bw. Dionis Ng’wandu ambaye wauaji hao walimcharanga mapanga sehemu za kichwani na kufariki dunia papo hapo.

Aidha aliyekatwa mguu wa kushoto amejulikana kwa jina moja la Bw. Themistocles  fundi ujenzi .
 
Kwa mujibu wa  Mchungaji wa kanisa hilo, Faustine Joseph, alisema baadhi ya waumini wa kanisa hilo wanadesturi ya kuomba hadi saa nne usiku.

Alisema kwa siku hiyo baada ya maombi waliamua kuondoka  majira ya saa 5:00 usiku  na kumuacha marehemu Bw. Ng’wangu  na mwenzake wakiendeleana mkesha wa maombi. 

Mchungaji Joseph,alisema  tukio hilo lilitokea  saa 8.00 usiku  ambapo alipigiwa simu  usiku huo na majirani wa eneo wanaoishi karibu na kanisani hapo.

'Nilipigiwa simu na mmoja wa majirani wa kanisa letu kuhusu watu wasiojulikana kuvamia waliokuwa kwenye maombi ya mkesha, nilipofika niliwakuta polisi wameshafika... kwa kweli hali inatisha sana"alisema.

Alisema katika uvamizi huo ambao ndiyo mara ya kwanza kutokea kanisani hapo watu hao hawakuiba kitu chochote hata simu zao walizokuwa nazo zaidi ya kufanya ukatili huo wa kutisha.

Hata hivyo, habari zaidi zinadai kuwa chanzo cha uvamizi huo unahusishwa na imani za kidini kwamba waliohusika na tukio hilo ni wapinzani wa dini hiyo.

Inadaiwa kuwa hadi wanatendewa kitendo hicho wahusika walikuwemo peke yao  majira ya saa 8 usiku baada ya wenzao kuondoka bada saa 4 usiku hivyo wao waliamua kulala kanisani.

Habari hizo zinadai kuwa mauaji ya mwalimu huyo yametokea  baada ya kuoa mwanamke wa dini nyingine na kumbadilisha dini.

Hatu hiyo inadaiwa kuwa iliwahudhi waumini wa dini ya mkewe ambao walianza vitimbi kwa kanisa hilo.

Kamanda wa polisi Mkoa wa kagera, Henry Mwaibambe ,alithibitisha kutokea kwa tukio hilo .
Alisema mwili wa mwalimu Ng'wangu umehifadhiwa katika hospitali ya mkoa Kaagera huku majeruhi wa tukio hilo amelazwa katika hospitali ya Mkoa Kagera kwa matibabu zaidi.

Alisema mtu mmoja ambaye hakuwa tayari kutaja jina lake anashikiliwa na Jeshi hilokwa mahojiano zaidi ambapo watu watatu wanatafutwa .



Thursday, October 9, 2014

Askari watatu watimuliwa kazi Kagera kwa kuendesha mapenzi kazini

Hii ndiyo picha ya kudahililisha Jeshi la Polisi Kagera iliosababisha  Maaskari  watatu kutimuliwa kazi. Picha hii matrafiki hawa wawili walipiga mwaka 2012  Wilaya ya Missenyi.

JESHI la Polisi mkoani Kagera limewafukuza kazi askari polisi watatu kwa kosa la kukosa maadili mema ya jeshi la Polisi.

Kamanda wa Jeshi la Polisi mkoani hapa Henry Mwaibambe,amewataja askari hiyo kuwa ni PC Asuma Mpaji Mwasumbi mwenye namba F.7788,PC Fadhiri Linga mwenye namba G 2122 na PC Veronica Nazaremo Mdeme,wote walikuwa askari wa kikosi cha usalama barabarani wilayani Missenyi.
 
Akifafanua tukio hilo,Mwaibambe amesema askari hao walitenda kosa hulo la fedheha kwa kupiga picha kinyume na maadili ya jeshi hilo mnamo mwaka 2012 wakiwa kazini,picha ambazo zimesambazwa sehemu mbalimbali za mitandao ya kijamii hapa nchini.
 
Alisema kuwa PC Fadhiri ndiye aliyehusika na kupiga picha hizo kwa kutumia simu yake ya kiganjani na kuituma katika mitandao mbalimbali ya kijamii kitendo ambacho ni kinyume cha maadili kwa sababu mbalimbali.
 
Amezitaja sababu hizo kuwa ni kupiga picha wakati wakijua kuwa kufanya hivyo ni kinyume cha maadili ya jeshi hilo pamoja na kuituma picha hiyo kwenye mitandao mbalimbali.
 
Aidha,Mwaibambe amekiri kuwa picha husika inayoonekana kwenye mitandao ni picha halisi ambayo haijachakachuliwa,hivyo ni wazi kila askari kujua kuwa maadili ya kijeshi yapo kisheria na askari yeyote anafundishwa namna ya kuishi katika maisha ya utumishi wa jeshi la Polisi.

Rais Kikwete akabidhiwa rasmi katiba iliyopendekezwa

2aMarais wote wa Tanzania Bara na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar wakikata utepe kufungua Katiba Inayopendekezwa wakati wa sherehe ya makabidhiano ya Katiba hiyo hapo jana 8 Oktoba, 2014 mjini Dodoma.(PICHA ZOTE NA BENEDICT LIWENGA, MAELEZO-DODOMA)3a
Marais wote wa Tanzania Bara na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar wakionyesha juu Katiba Inayopendekezwa ili wananchi waweze kuziona wakati wa sherehe ya makabidhiano ya Katiba hiyo hapo jana 8 Oktoba, 2014 mjini Dodoma.
 
4a
Rais wa Jamhuri ya Muungano ya Tanzania Dr. Jakaya Mrisho Kikwete  (kushoto) akikabidhiwa Katiba Inayopendekezwa toka kwa aliyekuwa Mwenyekiti wa Bunge Maalum la Katiba, Mhe. Samuel Sitta wakati wa sherehe ya Makabidhiano ya Katiba hiyo iliyofanyika jana 08 Oktoba, 2014 mjini Dodoma.
…………………………………………………………………..
Na Benedict Liwenga, Maelezo-Dodoma.
 
KATIBA Inayopendekezwa imekabidhiwa rasmi 8 Oktoba, 2014 kwa Waheshimiwa Marais wa Tanzania Bara, Mhe. Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete pamoja Rais wa Zanzibar, Mhe. Ali Mohammed Shein.
 
Akihutubia wakati wa sherehe ya Makabidhiano ya Katiba hiyo, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete alisema kuwa tukio hilo la kukabidhiwa Katiba Inayopendekezwa ni jambo la kihistoria kwa nchi ya Tanzania na linaashiria kukamilika rasmi kwa kazi ya lililokuwa Bunge Maalum la Katiba lililoanza tarehe 18 Februari mwaka huu.
 
Mhe. Dkt. Kikwete alisema kuwa ni hatua nyingine ya kihistoria ya nchi kwani hatua ambayo imesalia hivi sasa ni ile ya wananchi kwenda kuipigia kura za maoni Katiba hiyo ili waweze kufanya uamuzi kuhusiana na Katiba hiyo na endapo wananchi hao wataikubali basi Tanzania itakuwa imejipatia Katiba mpya ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
 
“Sina budi Kumshurkuru Mwenyezi Mungu kwa hapa tulipofikia na sina budi kumshukuru Mwenyekiti wa Bunge Maalum la Katiba, Mhe. Samuel John Sitta, Makamu wake Mama Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa na nzuri waliyoifanya, nawashukuru pia Wenyeviti wa Kamati mbalimbali za Bunge Maalum kwa uongozi waa makini, natoa pia shukurani za pekee kwa Wajumbe wote wa Bunge Maalum la Katiba kwa kukamilisha kazi hii tena mmeikamilisha kazi hii kwa kiwango cha juu sana cha ubora”, alisema Mhe. Dkt. Kikwete.    
 
“Shukurani zangu pia ziende kwa Katibu wa Bunge Maalum na Naibu Katibu pamoja na Wasaidizi wao wote kwa kazi nzuri walioifanya na kuiwezesha Bunge Maalum la Katiba kukamilisha kazi yake kwani haikuwa kazi rahisi hata kidogo”, aliongeza Mhe. Dkt. Kikwete.
 
Naye Rais wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Mhe. Dkt. Ali Mohammed Shein alimpongeza Rais wa Tanzania Bara, Mhe. Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete kwa kuanzisha mchakato huo wa kupata Katiba mpya na alitoa pongezi zake kwa Mwenyekiti wa lililokuwa Bunge Maalum la Katiba, Mhe. Samule Sitta pamoja na Makamu wake Mhe. Samia Suluhu ikiwemo pongezi pia kwa Wajumbe wote walioshiriki katika mchakato huo.
 
Katika Hotuba yake, Mhe. Dkt. Shein alisema kuwa katika mchakato mzima wa kutafuta Katiba hiyo, Zanzibar ilishirikishwa kikamilifu kwani hakuna hata hatua moja ambayo haikushiriki.
 
“Nataka leo nisisitize kuwa Zanzibar ibaki sehemu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika kila hatua ya mchakato huu imeshirikishwa na kushiriki kikamilifu hadi hivi leo tulipofikia”, alisema Dkt. Shein.
 
Naye aliyekuwa Mwenyekiti wa Kamati ya Uandishi wa lililokuwa Bunge Maalum la Katiba. Mhe. Andrew Chenge alisema kuwa ndani ya Katiba hiyo katika eneo la Uongozi, kwa mara ya kwanza katika historia ya Tanzania imeweka Ukomo wa idadi ya Mawaziri pamoja na Naibu Mawaziri ambapo kwa mapendekezo hayo, idadi ya Mawaziri na Naibu Mawaziri haitazidi 40.
 
Mhe. Chenge alifafanua kuwa idadi hiyo ya Mawaziri na Naibu Mawaziri itaisadia Serikali na Wananchi kupunguza gharama kwa ujumla na pia katika suala hilo hilo la uongozi aliongeza kuwa Rais wa Zanzibar anapokuwa Makamu wa Rais ni ishara ya Muungano, hivyo itaisadia Serikali ya Jamhuri ya Muungano kudumisha Muungano uliopo.
 
Aidha, Katika masuala yanayohusu Bunge, Chenge ameeleza kuwa Katiba inayopendekezwa inapendekeza mambo mawili ya msingi ambayo ni Uwiano wa Wabunge pamoja na Ukomo wa Idadi yao. 
 
“Kuhusu Uwiano wa Wabunge, inapendekezwa kuwepo na uwiano ulio sawa kati ya Wabunge Wanaume na Wabunge Wanawake uwe asilimia hamsini kwa hamsini”, alisema Chenge.
 
Akiongea kuhusu suala la ukomo wa Wabunge hao, wote wa kuchaguliwa na wale wa kuteuliwa, Mhe. Chenge alibainisha kuwa idadi hiyo haitapungua 340 na haitazidi 390.
 
“Mhe. Rais, Katiba hii Inayopendekezwa imesheheni malengo muhimu, ya Kiuchumi, ya Kisiasa, kijamii, ya kiutamaduni na kimazingira”, alisema Chenge.
 
Aliongeza kuwa katika malengo ya Taifa na kijamii yameboreshwa zaidi kwa kuweka mazingira yatakayowezesha Wasanii pamoja na Wanamichezo kukuza na kuendeleza vipaji vyao na kuleta mabadiliko ya kiuchumi katika jamii.

Sunday, October 5, 2014

Wakurugenzi na Maafisa elimu ambao ni walimu ndiyo vinara wa kuwanyanya walimu wenzao nchini-Pinda

Na Theonestina Juma, Kagera

Serikali imesema inaendelea kuboresha maslahi ya walimu nchini licha ya kukabiliwa na changamoto kubwa ya kiuchumi.

Hayo yamesemwa leo na Waziri Mkuu Mizengo Pinda kwa niaba ya Rais wa Tanzania Dkt. Jakaya Kikwete, wakati akihutubia katika kilele cha maadhimisho ya siku ya mwalimu duniani yaliofanyika katika Manispaa ya Bukoba.

Alisema kulingana na hali halisi ya walimu ndiyo inayoongoza kuwa na watumishi wengi katika kada zote hapa nchini, serikali inaendelea kuwaboreshea maslahi yao kulingana na hali ya uchumi wa nchi.

Halikadhalika Waziri Pinda aliahidi serikali kuwachukulia hatua kali za kisheria watumishi wa Halmashauri walioo ngeza takwimu katika madeni ya walimu wanaoidai serikali.

“Hawa watumishi walioamua kuingiza madeni hewa kwa kuongeza tarakimu mbele, lazima watafutwe na kuchukuliwa hatua kwa kuisababishia serikali hasara, kwani mwalimu mwenyewe anajua anadai serikali kiasi gani..”alisema.


Alisema Serikali ilibaini kuwepo kwa madai hewa ya sh.bilioni10.9,sh. billion 9 kutoka TAMISEMI na sh. bilioni 1.5 kutoka wizara ya elimu na mafunzo ya ufundi baada ya kukosa  viambatanisho  na vielelezo vya kuthibitisha uhalali wa madai hayohivyo kuonekana ni batili.

Katika hatua nyingine Waziri Mkuu alionesha kusikitishwa na  vitendo vinavyofanywa na baadhi ya wakuu wa idara wanaopandishwa vyeo kutokea sekta ya elimu kuwanyanyasa walimu wenzao pindi wanapohitaji msaada.

Alisema “ utendaji usioridhisha unasababishwa na baadhi ya walimu waliobahatika wakapata nafasi za Ukurugenzi na Afisa elimu kutowasikiliza walimu wake wakati matatizo yao wanayafahamu kwa nini hawa watu wanakuwa na roho mbaya kama hii”.

“Baadhi  ya Maafisa elimu ndio matatizo na taabu kwa walimu hawawezi kupitisha fomu za malipo ya uhamisho hadi wapewe hongo wakati na yeye ametoka huko huko… ni jambo la kusikitisha”aliongeza

Alisema walimu wanapofunga ndoa na kuomba kuwafuata wenzi wao wamekuwa wakizungushwa bila sababu za msingi.

“Kuna mambo mengine ni ya kushangaza waliotakiwa kuwasaidia walimu ndio wanageuka kuwa mbogo, mtu unamzungusha weee… hutaki amfuate mumewe hivi ni hawara yako?... hiyo ni roho mbaya” ninaikemea

Naye Naibu Waziri wa elimu na mafunzoya ufundi Bi.Jenister Muhagama, alisema sera ya elimu imeshakamilika itazinduliwa na Rais wowote na kwamba itahakikisha kuwa walimu wanaendelezwa kielimu.

Halikadhalika alibainisha kuwa bodi ya fani ya ualimu na Tume ya utumishi yameridhiwa na serikali kuanzishwa na ifikapo mwakani yatakuwa tayari kuanza kazi.
  
Kwa upande wa Katibu Mkuu wa Chama cha Walimu Tanzania (CWT) Alhaji Yahya Msulwa,alitoa zaidi ya mapendekezo 11 kwa ili kuwezesha kuboresha taaluma ya ualimu na maslahi ya watumishi na sekta ya elimu kiujumla.

Miongoni mwa mapendekezo hayo ni pamoja na serikali kurejesha posho ya ufundishaji kwani walimu ndiyo wanafanya kazi muda mrefu kuliko mtumishi yeyote hapa nchini na duniani kijumla.

Pia aliiomba serikali kuwajengea walimu nyumba za kulala kwa kushirikiana na wawekezaji kama Shirika la Nyumba  ambapo alibainisha kuwa kwa sasa kuna upungufu wa nyumba za walimu nchini 109,560 wakati nyumba zilizopo ni 55,000.

Halikadhalika aliiomba serikali kuwashirikisha kikamilifu walimu katika mabadiliko ya mitaala, kwani yanapofanyika bila kuwashirikisha walimu huaathiri kutokana na wao ndiyo watekelezaji wakuu wa mitaala hiyo.


mwisho

Pinda ni aibu kata moja kuwa na maprofesa zaidi ya 40 na wanafunzi wa eneo hilo kukosa madawati

DSCF3243*Yanahitajika madawati 99,204 kwa shule zote za msingi
WAZIRI MKUU Mizengo Pinda ameutaka uongozi wa mkoa wa Kagera ulichukulie suala la upungufu wa madawati kwa uzito ule ule kama ilivyo kwenye suala la ujenzi wa maabara katika shule za sekondari.
Ametoa wito huo jana usiku (Jumamosi, Oktoba 5, 2014) wakati akizungumza na viongozi na watendaji wa Serikali wa mkoa huo mara baada ya kupokea taarifa ya mkoa huo iliyowasilishwa kwake na Mkuu wa Mkoa huo, Kanali (Mst) Fabian Massawe.
Waziri Mkuu aliwasili Bukoba jana jioni akitokea Dodoma ili kumwakilisha Rais Jakaya Kikwete kwenye maadhimisho ya Siku ya Walimu Duniani ambayo kitaifa yanafanyika mkoani Kagera.
“Kwenye ujenzi wa maabara naona mnafanya vizuri lakini nataka kwa uzito uleule tusimamie suala la upungufu wa madawati. Tuunganishe nguvu za wananchi wa kawaida na za Serikali za Mitaa ili kuondoa kabisa tatizo hili mkoani mwenu,” alisema.
“RC hapa kasema kuna kata moja huko Bugandika kuna maprofesa 40. Huwezi kuwa na Maprofesa wote hao halafu kwenye shule wanakotoka maprofesa hao eti watoto wanakaa chini, haiwezekani!” alisisitiza.
Kwa mujibu wa taarifa kutoka ofisi ya Katibu Tawala wa mkoa huo, mkoa wa Kagera unahitaji madawati 238,080 kwa shule zote za msingi ambapo yaliyopo ni 138,876 na upungufu ni madawati 99,204. Kwa shule za sekondari, mkoa unahitaji viti 84,344, vilivyopo ni 82,275 na pungufu ni 2,069 wakati mahitaji ya meza ni 84,344; zilizopo ni 73,615 na upungufu ni 10,729.  
Aliwataka viongozi wa mkoa huo watafute mbinu za kukuza kipato cha wananchi wanaowaongoza kama njia mojawapo ya kuwasaidia wananchi wao kujikwamua kiuchumi. “Kwanza jiulize pato la mkoa likoje na limeongezeka kiasi gani? Je hali ya watu wangu ikoje? Nifanye nini ili niweze kuwaondoa hapo walipo na kuwafikisha katika kiwango kingine cha maendeleo?” alisisitiza
Alisema kama kila kiongozi atadhamiria kupambana na umaskini wa kipato wa wananchi, ni dhahiri kuwa kazi ya kuondoa maadui wengine ambao ni maradhi na ujinga itakuwa rahisi mno.
Mapema, akiwasilisha taarifa ya mkoa, Mkuu wa Mkoa wa Kagera, Kanali (Mst) Fabian Massawe alisema mkoa huo unahitaji kujenga maabara 570 ambapo zilizopo ni 136 wakati zingine 434 ziko katika hatua mbalimbali za ujenzi. Alisema mkoa unatumia maabara zinazohamishika (mobile labs) ambazo zipo 35.
Aliosema mkoa huo pia unazo hosteli za wananfunzi 84 na unahitaji kujenga hosteli nyingine 212 ili kuwasaidia watoto wa kike waweze kuhitimu masomo yao.
Akizungumzia hali ya ulinzi na usalama mkoani humo, Kanali Massawe alisema kati ya Desemba 2013 na Septemba 2014, jumla ya wahamiaji haramu 1,589 kutoka nchi jirani za Burundi, Rwanda Uganda na DRC wameondoshwa nchini na wengine 231 waliondoka kwa hiari ikiwa ni utekelezaji wa Operesheni Kimbunga Endelevu.
“Katika operesheni Kimbunga ya awali wahamiaji 25,258 waliondolewa nchini ikiwa ni sawa na asilimia 48 ya wahamiaji wote 50,520 wanaokadiriwa kuwepo mkoani Kagera. Tangu wakati huo, tumeendelea na misako kwenye mabasi, maeneo ya starehe, nyumba za kulala wageni, viwandani, mashambani, taasisi za elimu, taasisi za madhehebu ya kidini, vipenyo na vijiji vya mpakani.”
“Kuanzia Januari hadi Septemba mwaka huu, jumla ya watu 572 walikamatwa na kufikishwa mahakamani au kufukuzwa nchini (PI). Walioshtakiwa walikuwa ni 431 na kuhukumiwa vifungo ama kutozwa faini na wahamiaji 231 walifukuzwa nchini kwa PI,” alifafanua.