RORYA KWETU

Pata habari moto moto kila siku, kwa Mawasiliano zaidi piga Simu Na. 0755 856991/ 0712 992434 Email:-theonestinajuma@yahoo.com/rorya.09@gmail.com

Monday, April 30, 2012

Yaliopita si ndwele, lakini.... Ati wanabeza lugha yetu iliotuunganisha na kuwa kitu kimoja miaka nenda rudi!

Na Theonestina Juma, Uganda
KUTOKANA na baadhi ya viongozi wa nchini Uganda kudai kuwa hawajisikii vizuri Kiswahili kutumika katika mazungumzo ya Ushirikiano wa Jumiya ya Afrika Mashariki katika mkutano uliotangulia juzi iliwalazimu kukaa kimya baada ya viongozi kutoka Tanzania kukitumia lugha hiyo kuanzia mwanzo hadi mwisho wa majadiliano.
Hayo yalibainika Oktoba 24, mwaka 2011 katika mkutano wa hadhara uliofanyika katika uwanja wa mpira wa Malaba wilaya ya Rakai nchini Uganda, uliohudhuriwa na Naibu wa Waziri Mkuu ambaye pia ni Waziri wa Shirikisho la Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) nchini humo, Bw. Eriya Kategaya ambaye ndiye alikuwa mgeni rasmi, pamoja na ujumbe kutoka Tanzania ulioongozwa na Naibu Waziri wa (EAC) wa Tanzania, Bw. Abdallah Sadallah.
Katika Mkutano huo, ambao mtu wa kwanza kuzunguza na wananchi katike eneo hilo alikuwa ni Mkuu wa Mkoa Kagera, Kanali Fabian Massawe ambaye katika utambulisho wake alilazimika kujibu mapigo kwa kutumia lugha ya Kiswahili bila kuchang’anya na lugha ya kiingereza katika mkutano wake wote.
Akizungumza katika mkutano huo, Kanali Massawe alisema lugha ni kitu muhimu na ili waweze kushirikiana ni lazima itafutwe lugha moja itakayotumiwa katika mawasiliano na kuelewana tofauti na hivi sasa, ambapo kunajitokeza mkanganyiko.
“Lugha ni kitu muhimu na ya msingi sana katika mawasiliano, na ili tuweze tushirikiane, itafutwe lugha moja ya mawasiliano hata kama ni Acholi, Kiganda, kihaya …..lakini mambo ya kutumia makalimani ni kuonesha udhaifu wa ushirikiano wetu”alisema.
Alisema iwapo itapatikana lugha yoyote moja itakayokubalika kutumika jumuiya hiyo wananchi pamoja na viongozi wao hawana budi kukijifunza kwa bidii, kwa ajili ya maendeleo yao.
“Hebu angalieni Wazungu mfano kama Marekani wanatumia lugha gani kuu ya mawasiliano… wao wamechagua lugha moja ya mawasiliano na ndiyo maana wameweza kupiga hatua”aliongeza.
Hata hivyo, aliwaomba viongozi wanchi hizo kutumia vyombo vya habari vya kijamii vilivyoko mikoani katika kuelimisha wanachi juu ya shirikisho hilo kwani vyombo hivyo navyo vina nguvu katika jamii inayowazunguka.
Naye Naibu Waziri Mkuu wa nchini humo, Bw. Kategaya akizungumzia historia ya Kiswahili nchini Uganda alisema wananchi wengi wao wanajua kuwa Kiswahili ni lugha ya majambazi wanaopora mali za wananchi na askari wanaoitumia kwa kutoa amri hali iliowajengea woga wananchi na kukichukia.
Alisema licha ya lugha ya Kiswahili kuchukuliwa kwa mtizamo huo, lakini katika kiserikali ni lugha ya mawasiliano na ni lugha kuu inayotumiwa na watu wengi wa Afrika Mashariki.
Alisema pamoja na hali hiyo, kupitia wizara yake na ya elimu nchini humo, unafanya mpango ambapo hadi kufika mwakani lugha hiyo itaanza kufundishwa kuanzia elimu ya msingi lengo likiwa ni kutaka kukiendeleza ili wananchi wa nchini humo waweze kukielewa katika mawasiliano.
Katika kikao kilichofanyika juzi nchini humo katika ukumbi wa Juuko’s wilayani Rakai baadhi ya viongozi wa nchini humo, wakioongozwa na Mkurugenzi (CHO) wa wilaya hiyo,Nkato James  walionesha wazi kukibeza lugha ya Kiswahili ambayo ni lugha ya saba duniani kwa madai kuwa hawajisikii vizuri kukizungumza, ambapo walitaka lugha ya kiingereza na kiganda ndizo zitumike.
Katika mkutano huo wa siku mbili ulilenga  kujadili masuala ya ushirikiano wa jumuiya ya Afrika Mashariki, mafanikio, fursa na changamoto zinazozikabili nchi wananchama kati ya Tanzania na Uganda kwa upande wa maeneo ya mipakani.
Mwisho.


Posted by www.theonestinaj.blogspot.com at 3:48:00 PM No comments:
Email ThisBlogThis!Share to XShare to FacebookShare to Pinterest

Kwa wenzetu wa nchi jirani ya Uganda usalama uko hivi

Ndugu yangu eh kuingia humu ni kwa kufuata mstari maalum usidhani uko TZ, hawa ni baadhi ya wananchi waliokuwa wakihudhuria katika mkutano wa kujadili  Shirikisho laJumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) kati ya Tanzania na Uganda wakikaguliwa kwa kifaa maalum, kabla ya kuingia uwanja wa mpira wa Malaba wilayani Rakai Nchini Uganda, anayekaguliwa  na polisi huyo wa Uganda ni Mwandishi wa gazeti la Mwananchi Mkoani Kagera, Bw. Phinias Bashaya.
 Wee..panga mstari Bwana, mbona kana kwamba uko nje ya mstari ndivyo inavyoonekana huyu askari wa nchini Uganda akimwambia mtu anayetazamana naye.
 Haya , ukaguzi kwa kutumia kifaa maalum ukiwa umepamba moto kwa wageni waalikwa wa mkutano huo.
Baadhi ya viongozi wa pande zote mbili Uganda na Tanzania wakiwa katika picha ya pamoja, wa tano kutoka upande wa kushoto ni Naibu Waziri Mkuu ambaye pia ni Waziri wa EAC nchini Uganda, Bw. Eriya Kategaya, wa kwanza upande wa kushoto ni Mkuu wa Mkoa Kagera Kanali Fabian Massawe, wa kwanza upande wa kulia ni Mkuu wa Wilaya ya Bukoba, anayemfuatia ni Naibu Waziri wa EAC Tanzania, Dkt. Abdallah Sadallah na anayemfuatia wa tatu kutoka kulia ni Mkuu wa wilaya ya Missenyi, Kanali Issa Njiku.
Jamani bado mnaendelea kuchukua sura zetu, mmmh hawa ni viongozi hao katika picha ya pamoja.
Posted by www.theonestinaj.blogspot.com at 3:36:00 PM No comments:
Email ThisBlogThis!Share to XShare to FacebookShare to Pinterest

Uwepo wa Mungu unapoonekana hivi.......Mugana.

 Mamia wa waumini wa Kanisa Katoliki kutoka ndani na nje ya nchi, wakiwa katika Parokia ya Mugana ambapo Oktoba 30, kila mwaka hufurika katika eneo hilo kuhiji.Waliovaa mavazi meupe katikati ya umati wa watu, ni Mapadri wa kanisa hilo kutoka ndani na nje ya nchi.
Utukufu kwa Mungu juu mbinguni, hivi ndivyo hali inavyokuwa Oktoba 30 kila mwaka, katika kituo cha kuhiji cha Mugana Wilayani Missenyi, ambapo idadi ya watu wanaojitokeza hawahesabiki, lakini cha ajabu watu wanaofika katika hili wanakuwa watakatifu kweli, kwani hata vibaka hawaonekani kwani kila mmoja anakuwa na mshike mshike wake wa kutaka kuondoka na maji ya baraka.(Picha zote na Theonestina Juma)

Posted by www.theonestinaj.blogspot.com at 11:36:00 AM No comments:
Email ThisBlogThis!Share to XShare to FacebookShare to Pinterest

Mambo yote ni sawa ilimradi tuvuke salama.

Mumiliki wa blog hii, Bi.Theonestina Juma, akivuka mto Ruvuvu unaoungana na mto Rusumo ulioko mpakani mwa Tanzania na Rwanda.Maji ya mto huu kwa kawaida mtu akiyatazama kwa macho ni kana kwamba yamesimama wala hayaendi, lakini kwa watafiti wa masuala ya maji wanadai kuwa maji hayo yanakasi ya ajabu.
Posted by www.theonestinaj.blogspot.com at 10:56:00 AM No comments:
Email ThisBlogThis!Share to XShare to FacebookShare to Pinterest

Amani na maendeleo... Kagera, Kagera... Amani na Maendeleo




 Mkuu wa mkoa Kagera, Kanali Fabian Massawe akihutubia Wajumbe wa Mkutano (hawako pichani) Mkuu wa 25 wa Chama cha Ushirika Wilaya ya Karagwe Ltd (KDCU) katika Ukumbi wa CCM Wilayanni  humo.Picha ni kwa hisani ya Afisa Habari Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Kagera,(Raphael Sylvester)
Posted by www.theonestinaj.blogspot.com at 10:08:00 AM No comments:
Email ThisBlogThis!Share to XShare to FacebookShare to Pinterest

'Hatuondoki, hata kama mkiwaleta kikosi cha FFU'-Wafanyabiashara Soko Kuu Bukoba

UJENZI wa soko kuu la kisasa katika Manispaa ya Bukoba huenda' ukaingiwa na mchanga' kutokana na wafanyabiashara wote wa  soko hilo kusema kuwa hawako tayari kuondoka humo kupisha ujenzi huo.
Wafanyabiashara hao walifikia uamuzi huo juzi katika mkutano wao wauliofanyika ndani ya soko hilo kujadili hatma yao baada ya kuondoka ndani ya soko hilo kupisha ujenzi kuanza.
Wafanyabiashara hao waliokuwa wakizungumza kwa jazba walidai kuwa hawajashirikishwa kikamilifu na ujongozi wa Manispaa ya Bukoba juu ya ujenzi wa soko hilo la kisasa tangu mwanzo ambapo kwa sasa ndiyo wanashang'aa wakielezwa kutakiwa kuondoka sokoni hapo kupisha ujenzi wake ambao utagharamu kiasi cha sh. bilioni 11.
Hao wanaotuambia kuwa tuondoke ndani ya soko, twende wapi... wakati sisi baadhi yetu wamekopa fedha katika taasisi mbali mbali za fedha kama FINCA, CRADB, sasa tutatoa wapi fedha za kurejesha? Tunawatoto watutegemea, kila kitu ndani kinaangalia hii kazi yetu tutaenda wapi? alisikika mmoja wa wafanyabiashara ndani ya soko hilo alihoji.
Wafanyabiashara hao walidai kuwa wanashangazwa kuona miradi mitatu mikubwa yanatekelezwa kwa mkupuo ndani ya Manispaa ya Bukoba, bila mpangilio unaoeleweka kwa wananchi ambapo kwa mawazo yao walishauri kuwa itekelezwe mradi moja baada ya nyingine.
Walisema wao wanashang'aa kumsikia Mstahiki Meya  wa Manispaa ya Bukoba, Dkt. Anatory Amani akizungumza kupitia redioni kuhusiana na ujenzi wa soko hilo na kutakiwa wao wafanyabiashara kuondoka kupisha ujenzi huo bila kwenda kwao kuzungumza nao.
Miradi mkubwa inayotarajiwa kuanza kutekelezwa na Manispaa ya Bukoba ni pamoja na ujenzi wa jengo la kitega uchumi ghorofa 10, itakayogharimu kiasi cha sh. bilioni 20, ujenzi wa kituo cha mabasi sh. bilioni 1 na  ujenzi wa barabara za lami sh. bilioni 6.
Katika kikao cha dharura cha Baraza la Madiwani wa Manispaa ya Bukoba kilichofanyikaAprili 16 mwaka huu, kiliafikia kuanza kwa ujenzi wa soko hilo, ili kuwezesha mji wa Bukoba kuweza kuonekana tofauti na miaka mingine kutokana na kuwa kongwe lakini maendeleo ikiwa ni ZERO.
Hata hivyo, katika uchunguzi wa blog hii umebaini kuwepo kwa kundi la watu wasioitakia maendeleo Manispaa ya Bukoba, ambapo tatizo lingine likiwa ni baadhi ya viongozi walioko madarakani pamoja na baadhi ya wanasiasa kupingana wenyewe kwa wenyewe kwa ubinafsi tu.
Katika kikao cha Baraza la Madiwani, Kaimu Mkurugenzi wa Manispaa ya Bukoba, Bw. Robert Kwela, aliwaambia Madiwani hao kuwa tayari yameshafanyika mazungumzo zaidi ya mara mbili kati ya uongozi wa Manispaa na wafanyabiashara hao, namna watakavyoweza kupisha ujenzi huo kwa kutawanyika katika baadhi ya masoko yalioko mjini hapa.
mwisho.


Posted by www.theonestinaj.blogspot.com at 3:41:00 AM No comments:
Email ThisBlogThis!Share to XShare to FacebookShare to Pinterest

Friday, April 27, 2012

Mmoja wa wajumbe wa mkutano mkuu wa mezania wa Chama cha Ushirika wa mkoani Kagera(KCU)1990 Ltd akizungumza katika mkutano huo.Katika mkutano huo, wajumbe hao walihoji inakuwaje hoteli yao ya Lake iingize faida ya sh. milioni 1,000,300 tu kwa mwaka wakati mtaji ikiwa ni sh. milioni 86.


Posted by www.theonestinaj.blogspot.com at 6:48:00 AM No comments:
Email ThisBlogThis!Share to XShare to FacebookShare to Pinterest

Thursday, April 26, 2012

Hapo vipi?

 Aliyesimama upande wa kushoto ni mumiliki wa blog hii (Theonestina Juma)akiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya ndugu zake, ambao ni Happiness Odira, aliyevaa fulana ya njano na anayemfuatia ni Euphrasia Juma, tukiwa tayari kushiriki kikamilifu katika mambo fulani za kimila huko kijijini kwetu, Rorya Mara.
 Mkuu wa mkoa wa Kagera, Kanali Fabian Massawe aliyesimama nyuma ya baadhi ya wanahabari  ofisini kwake akiwa amebeba mkononi kinasa sauti kwa lengo la kuwawezesha waandishi wa habari kusikiliza wimbo maalum aliourekedi, uliotungwa na kuimbwa na bandi la Kakau (Kanisa Katoliki na Ukimwi) mjini  Bukoba kwa ajili ya kuhamasisha maendeleo ya Mkoa wa Kagera.
 Kamanda wa Polisi Mkoani Kagera, Henry Salewi akiangalia kwa makini pombe iliotengenezwa kwa ndizi maarufu kama 'banana Wine' katika maonesho ya siku ya mkulima wa migomba Mkoa wa Kagera.Kinywaji hiki kinadaiwa kuwa na kilevi asilimia saba.
Profesa Swenner Rony huyo mzungu aliyesimama na kuvaa shati nyeupe, kutoka chuo kikuu cha Leuven nchini Ubelgiji aliyesaidia kuboresha mradi kiutaalam na ushauri katika kuendeleza zao la Migomba mkoani Kagera akiwa anakula balagara iliotengezwa kwa ndizi, hapa alikuwa katika maonesho ya siku ya zao la migomba mkoa Kagera yaliofanyika wilayani Ngara.
Posted by www.theonestinaj.blogspot.com at 11:06:00 AM No comments:
Email ThisBlogThis!Share to XShare to FacebookShare to Pinterest

Leo ni siku yangu ya kuzaliwa, asante Mungu kwa kunibariki.

Leo ni Aprili 26,2012, ninatimiza MIAKA kadhaa ya kuzaliwa.Namshukuru sana Mungu wangu muumba wa mbingu na nchi na kila kitu kilichomo hapa duniani, kwa kuniwezesha kufika hadi siku hii ya LEO.
Nashindwa hata namna ya kumshukuru Mungu kwani sielewi ni kwa nini bado ananipa pumzi ya kuvuta hewa ya dunia hii.Lakini katika hili najipa moyo na kuamini ni jinsi gani pendo la MUNGU HALICHUJI na  Pendo lake lilivyo la milele, bado ananipenda!, bado ananihitaji nielendelee kuishi katika uso wa dunia hii.
Siku kama hii ya leo, mama yangu aliyenizaa hawezi kusema ni namna gani labda mimba yangu ilivyomsumbua, lakini kwa uwezo wa Mungu nilizaliwa salama salimini.
Oh, Mungu wa Upendo naomba uendelee kunipa baraka zako ziniwezeshe kuendelea kukupenda kwani hapa duniani kumejaa vishawishi vingi, kupitia SHETANI Mwovu anayerandaranda kila kona za nyoyo za Wanadamu ili wamfuate.Lakini naamini kwa jina lako TAKATIFU utaniepusha na vishawishi vya huyo IBILISI.
Mungu niepushe na wale binadamu wenye roho za kishetani, wanaochukia binadamu wenzao bila sababu zozote za msingi, niepushe na binadamu wasio kuwa na moyo wa ustahimilivu, niepushe na wanadamu wasio penda maendeleo na wenzao.Niepushe na binadamu wasengenyao wenzao,waliojaa hila,wasiopenda wenzao wapate.Niepushe ni watu wanaojipenda wenyewe zaidi ya wenzao, wanaojiona wao ndiyo bora kuliko viumbe vyako vingine hapa duniani.
Mungu tujalie uwezo na nguvu za kupendana sisi wanadamu, imarisha upendo kati ya familia yangu, ukoo wafanyakazi wenzagu N.K.
MUNGU ibariki nchi yangu Tanzania, nuru yako iwake na ing'arishe wa wale wote wanaokuchaa.
Aksante Mola kwa kuzidi kunipenda, pendo lako linazidi kunipo faraja ya kuendelea kuishi hapa dunia na kuzidi kukutumikia.AMENA.
 

Posted by www.theonestinaj.blogspot.com at 1:06:00 AM No comments:
Email ThisBlogThis!Share to XShare to FacebookShare to Pinterest

Wednesday, April 25, 2012

Ati anamsafirisha Simba kwenye baiskeli!

 
Kweli angekuwa Simba halisi hata kama ni mdogo kiasi gani sidhani kama angekubali chakula chake kumsafirisha kwa mtindo huu.
Posted by www.theonestinaj.blogspot.com at 11:37:00 AM No comments:
Email ThisBlogThis!Share to XShare to FacebookShare to Pinterest

Tudumishe mila zetu.

 Hawa ni baadhi ya wajukuu, wakiwa porini wakimburia Mzee Alloyce Amworo (90)  wakiwa wamejipumzisha porini wakifunga bendera, pamoja na vitu vingine huku ng'ombe hawako pichani wakielendea kupata majani.Kuburu ni kitendo cha kuswaga ng'ombe wa marehemu pamoja na wana ukoo na kupelekwa kwenye malisho huku wakipiga ngoma na kuimba mbali na mji wa mtu aliyefariki, ambaye mara nyigi huwa ni mwanaume aliyeoa na kuacha mji wake kulingana na mila na desturi za kabila la Waluo, hatua hii inakuwa ya mwisho ikiwa ni siku ya kuanua matanga.Kwa kawaida wajukuu wakiume na na wakike pamoja na wasichana wa ukoo huo walioolewa ndiyo huwajibika kufanya shughuli hiyo, ambapo hulazimika kuondoka msibani asubuhi kuanzia saa 1.Na hutakiwa kurejesha mifugo hao kuanzia saa tisa alasiri na kuelendelea.Ni lazima kuwepo kwa bendera za khanga zinazofungwa na wanawake.
 Baadhi ya wajukuu waliokuwa wakikabiliwa na shughuli maalum ya kuburu kwenye msiba wa babu yao wakiwa katika picha ya pamoja na mumili wa Blog hii aliyevaa kitambaa cheusi shingoni.Hapa wakiwa tayari kuelekea msibani wakiwa wamejifunga majani hayo maalum kwa ajili ya shughuli hiyo pamoja na kujipakaa na kujichora mwilini kwa kutumia udongo maalum ambao mara nyingi hupatikana maeneo ya mito.
Hapa baadhi ya wabururaji wakiwa kwenye kaburi la Mzsee wetu wakibaki kushang'aa yanayotokea katika tukio hilo.
Posted by www.theonestinaj.blogspot.com at 7:14:00 AM No comments:
Email ThisBlogThis!Share to XShare to FacebookShare to Pinterest

Tuesday, April 24, 2012

Wajumbe wa mkutano Mkuu KCU 1990 Ltd wapigwa mbumbuwazi faida sh. milioni 1 kwa mwaka mtaji sh.milioni 86!


Bukoba
WAJUMBE wa mkutano mkuu wa Chama cha Ushirika wa Kagera (KCU) 1990 Ltd wamesikitishwa na mradi wao wa hoteli ya Lake kuzalisha sh. milioni moja tu kwa mwaka wakati mtaji ukiwa ni sh. milioni 86.
Wajumbe hao walionesha kusikitishwa na kiasi hicho, katika Mkutano wa Mkuu wa Mizania ya mwaka 2010/2011 wa Ushirika huo uliofanyika katika hoteli yao ya Coop walionunua kwa zaidi ya sh. milioni 300 takribani miaka mwili iliopita ilioko kando kando ya ziwa Victoria mjini Bukoba.
Wajumbe hao walisema haiwezekani kwa mwaka mtu apate sh. milioni 1,000,300 huku mtaji wake ukiwa ni sh. milioni 86 hivyo inahitaji kuangaliwa suala hilo kwa makini.
Hapa kuna tatizo pale wanauza nyama choma, bia, soda na kuna baadhi ya wageni wanalala humo iweje ipatikanaje kiasi hicho, inamaana kila mwezi wanafanyia faida ya sh. 25,000?alihoji Mjumbe mmoja kutoka katika Chama cha msingi ha Tukutuku wilayani Muleba.
Mjumbe huyo alisema inawatia wasi wasi juu ya kiasi hicho, ambapo alitoa angalizo kwa uongozi wa Ushirika huo, kuangalia kama kweli watendaji wanaofanya kazi hotelini hapo wanafanya kazi kweli ama la.
“Kuna hatari hapa, Wataalam waliowekwa katika mradi huu, wapo kwa ajili ya maslahi yao binafsi au vipi?alihoji tena mjumbe huyo.
Alimtaka Mwenyekiti wa Ushirika huo, Bw. John Binunshu ambaye anatoka katika Chama cha msingi cha Muhutwe Muleba, asimamie kikamilifu mradi wa hoteli ili iweze kuzalisha kile wanachokitegemea na si fedha za wakulima wa kahawa kupotea bure.
Hata hivyo, kwa upande wa Meneja wa (KCU 1990) Ltd Bw. Vedasto Ngaiza akijibu malalamiko ya baadhi ya wajumbe hao alisema faida ndogo iliopatikana katika hoteli hiyo inatokana na mapungufu makubwa ilinayo hoteli hiyo tofauti na hoteli zingine zilizopo mjini Bukoba licha ya kuwa kongwe.
Alisema huduma zinazotolewa katika hoteli hiyo ni hafifu, na hivyo inahitajika kuboreshwa zaidi ili kuweza kushindana na hoteli zingine nyingi zilizoko mjini hapa.
“Kwa sasa Bukoba kuna hoteli nyingi sana, zimeboreshwa  na kuwa katika viwango vya juu, tofauti na hoteli yetu licha ya kuwa kongwe, ambapo fedha ambazo zilitengwa  mwaka jana kwa ajili ya kuiboresha ililazimika zitumike kwenye ujenzi wa nyumba nyingine ambayo pia ikikamilika itakuwa ni kitega uchumi nzuri kwa wakulima”alisema Bw. Ngaiza.
Mwisho.

Posted by www.theonestinaj.blogspot.com at 2:16:00 PM No comments:
Email ThisBlogThis!Share to XShare to FacebookShare to Pinterest

Monday, April 23, 2012

Elizabeth 'Lulu' apandishwa tena kizimbani, sasa aongezewa ulinzi

Mshatkiwa Elizabeth Michael |(17), ' Lulu'  akielekea kupanda ngazi na kupandishwa Kizimbani Kesi hiyo  ilikuja kwa ajili ya kutajwa  Upelelezi haujakamilika hiyo ni kwa mujibu wa Wakili wa Serikali Elizabeth Kaganda alisema mbele ya Hakimu Mkazi wa Mahakama hiyo Rita Tarimo  hivyo kesi hiyo  itatajwa tena Mei 7 mwaka huu. Mtuhumiwa amerudishwa rumande.
 Akizindikizwa ndani ya chumba cha Mahakama ya hakimu mkazi kisutu jijini Dar es Salaam leo
Mshtakiwa akipanda ngazi kuelekea Kizimbani ambalo kesi yake ilitajwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Jijini Dar es Salaam huku akiwa katika ulinzi mkali kutoka kwa askari  Magereza.Picha na Mdau Khadija Kalili
Posted by www.theonestinaj.blogspot.com at 10:27:00 AM No comments:
Email ThisBlogThis!Share to XShare to FacebookShare to Pinterest

Upumzike kwa amani Mzee wetu Mpendwa.

 Misa takatifu ilianzia katika kigango cha Bugando Jijini Mwanza ya kuaga mwili wa mzee Allyoce Amworo.
 Mwili wa Mzee wetu ukiwa ndani ya jeneza
 Msururu wa magari yakisindikiza mwili wa marehemu Amworo kwenda kuombea misa takatafu parikia ya Ingri Rorya
Baada ya Maziko mzee huyu maarufu katika wilaya ya Rorya kwa jina la Kapila akiwaburudisha  baadhi ya waombolezaji kwa kusakata rumba.
Posted by www.theonestinaj.blogspot.com at 4:28:00 AM No comments:
Email ThisBlogThis!Share to XShare to FacebookShare to Pinterest

Sunday, April 22, 2012

"Babu tulikupenda sana, kwa kheri"

  Mchungaji wa Kanisa la Anglikana  Jimbo la Musoma,Gasper Kasanda Amworo akisoma wasifu wa marehemu Mzee Alloyce Amworo (90) katika Misa Takatifu iliofanyika katika Kanisa Katoliki Parokia ya Ingri.
 Mchungaji Kasanda akiwa sambamba na mke wa marehemu kaka yake Alloyce  na shemeji yake marehemu, Bi. Aoko wakiongozana kuingia kanisani katika misa ya kumwombea marehemu.
 Fundi akisakafikia kaburi muda mfupi kabla Marehemu Alloyce kupumzishwa humo, hapa ni kijiji kwake Randa, Kata Kigunga Wilayani Rorya
 Padri wa Kanisa katoliki Parokia ya Ingri, Romanus Ciupaka akiangaliajeneza lililobeba mwili wa marehemu Mzee Alloyce Amworo (90) ukishushwa ndani ya gari kwa ajili ya kuingizwa kanisani huku akipokea tayari kuupokea na kuuombea tayari kurejeshwa nyumbani kwake kwa ajili ya kuhifadhiwa katika nyumba yake ya milele.
 Baadhi ya waombolezaji waliohudhiria katika mazishi ya Mzee Alloyce Amworo kijijini kwake.
 Mmiliki wa Blogi hii aliyesimama akibofya simu yake, akiwa msibani hapo.
 Sehemu ya wanakwaya wakiimba ndani ya kanisa.
 Baadhi ya wajukuu, na wakwe wa marehemu wakiwa katika picha ya pamoja na dada wa marehemu, aliyekaa kwenye kiti akiwa amebeba chupa ya maji mkononi, Bi. Magreth Amworo(97) muda mfupi baada ya kuwasili kutoka nchini Kenya alikoolewa.
Hawa ni baadhi ya ndugu wa mke wa marehemu wakiwa wanamliza wakiwa jijini mwanza kabla ya maiti kusafirishwa kwenda Mara, Rorya.
Posted by www.theonestinaj.blogspot.com at 6:19:00 AM No comments:
Email ThisBlogThis!Share to XShare to FacebookShare to Pinterest

Matukio katika picha.

 Ndizi aina ya gonja iyoliwa ikiwa imechomwa kwenye moto au mafuta ya kupikia.
 Mkulima wa migomba aina ya FHIA wa kijiji cha Kasulo Wilayani Ngaram, Bw. Samuel Kaparala akiwa katika maadhimisho ya siku ya migomba Mkoa Kagera.
 Pori la Kimisi iliokuwa ikitumiwa na majambazi kujificha wakati wakiteka magari ya abiria, pori hili kwa sasa magari yanapita bila kusindikizwa na askari polisi kama ilivyokuwa miaka ya nyuma kabla ya ujio wa Kamanda Tossi.
 Mkuu wa Mkoa wa Kagera, Kanali Fabian Massawe mwenye tai jekundu akisiliza maelezo kutoka kwa Mratibu wa zao la Migomba Taifa, Bw. Mugenzi Byabachwezi namna ya kutunza zao la migomba wa pili upande wa mkono wa kushoto ni Mkuu wa Wilaya ya Ngara, Kanali Salum Nyakonji.
 Taswira katika Taifa, hawa ni baadhi ya watoto wa kijiji cha Rusumo waliohudhuria katika maadhimisho ya siku ya mgomba Kagera yaliofanyika hapo kijijini kwao.
 Kikundi cha Mshikamano kinachojishughulisha na kilimo cha migomba ya kisasa wakicheza ngoma katika maadhimisho ya siku yao.Tangu miaka 750 iliopita hakujawahi kuwepo maadhimisho ya siku ya migomba nchini, wala duniani.Haya ni maadhimisho ya kwanza ya siku ya migomba kufanyika hapa nchini, ndani ya mkoa wa Kagera Wilayani Ngara.


Posted by www.theonestinaj.blogspot.com at 4:01:00 AM No comments:
Email ThisBlogThis!Share to XShare to FacebookShare to Pinterest

Sijaamini kama nimetoka hai katika ajali hii.

 Hiki ni choo cha shule ya sekondari  ya Omumwani inayomilikiwa na Umoja wa Wazazi Tanzania CCM,Mkoa wa Kagera kilichototia Machi 4, mwaka huu saa 2.00 akiwemo mwanafunzi wa kidato cha tatu, Edwin Adam aliyekuwa akijisaidia.Mtoto Adam aliweza kuokolewa na wapishi wa shule hiyo kwa kushirikiana na uongozi wa shule.

Bukoba
MWANAFUNZI wa kidato cha tatu katika shule ya Sekondari ya Omumwani ,inayomilikiwa na Umoja wa wazazi Tanzania (CCM) katika Manispaa ya Bukoba,  Edwin Adam (16) amenusurika kufa baada ya choo cha bweni la wanaume kutitia chini akiwa ndani akijisaidia.
Tukio hilo la kusikitisha na la aina yake  tangu mwaka huu uanze , na kuacha simulizi ya kipekee shuleni hapo lilitokea Machi 4, mwaka huu saa mbili asubuhi, ilioambatana na mvua kubwa ilioanza kunyesha mjini hapa kuanzia saa 11 alfajiri hadi saa 6 mchana.
“Ni kumsuhukuru Mungu, na ni miujiza tu, kama kweli mtu ameweza  kutoka akiwa hai katika tukio hili…, kweli Mungu ni mkubwa kama  mtoto Adam ametoka akiwa hai…..inasikitisha… sijawahi kuona”alisema Mkuu wa shule hiyo, Bw. Modest Byeshulilo.
Akizungumza na gazeti shuleni hapo, mwanafunzi Adam ambaye ni mwenyeji wa wilaya ya Rorya Mkoani Mara, alisema wakati tukio hilo lilitokea, alikwenda chooni akiwa na wanafunzi wenzake, ambapo walijisadia na yeye akabaki kutokana na wiki hiyo nzima alikuwa akisumbuliwa na ugonjwa wa malaria  pia na tumbo la kuharisha.
Alisema alikaa takribani dakika tano, ambapo alisikia kitu kama tetemeko ndani ya tundu la choo alilokuwemo, jambo ambalo lilimshutua na hivyo kunyanyuka haraka na kuanza kufunga ‘pensi’ lake, na alipotaka kuondoka tu, ghafla asikia kishindo, cha kitu kizito, mbele yake kumbe ulikuwa ni paa  la jengo la choo hicho ambalo lilidondokea mbele ya  mlango alikokuwa akitaka kutokea na ukazibwa kabisa.
“Nashindwa hata kupata namna ya kuelezea kwa kweli…., choo hakikuwa na hitalafu yoyote kimtazamo wangu,…. lakini ninachokumbuka nikiwa ndani ya choo tundu namba  tatu mkono wa kushoto ukitokea bwenini kwetu, baada ya kubaki peke yangu, nilisikia tundu la choo nilichokuwemo likitikisika  kama vile tetemeko, jambo lililonifanya kuingiliwa na wasi wasi kwani si kawaida na kunyanyuka haraka  na kuanza kufunga ‘pensi’ langu ili niondoke”
“Lakini baada ya kumaliza  nilipoanza tu kuondoka chooni, mara nilisikia kishindo cha kitu mbele ya mlango niliokuwa nikitaka kupitia, bila kufahamu ni nini, mara nilianza kusikia vitu  vigumu vigumu  vikinidondokea  mwilini  kwa nguvu kutoka juu kama vile mawe mawe, mara nikaonekana ninatumbikia shimoni nikalazimika kushikilia nondo , ambalo nalo hatimaye kana kwamba sijui ilikatika….ndipo nikajua kuwa kumbe niko kwenye kifo” alisema mtoto Adam.
Hata hivyo, kutokana  tukio, wapishi waliokuwa karibu na eneo la tukio hilo ndiyo waliwahi kufika hapo kuokoa maisha ya mwanafunzi huyo kwa kutumia ngazi,  kwani kwa wakati huo tayari baadhi ya sehemu ya kuta za choo hicho kilishabomoka na kutitia ndani ya choo hicho  na mtoto huyo akiwa hatarini kufunikwa na kifusi cha ukuta wa choo hicho kilichokuwa kikibomoka na kutumbukia ndani ya choo hicho.
Akizungumza na gazeti hili, Mkuu wa shule hiyo, Bw. Byeshulilo alisema , katika tukio hilo, miujiza iliofanyika ya kuokoa maisha ya kijana huyo, ni ya kipekee kwani haijulikani jinsi ilivyotokea, ya sehemu ya ukuta wa choo hicho kutanguliwa chini na kufuatiwa na upande wa tundu la choo alichokuwemo mwanafunzi huyo, kuangukia juu ya ukuta huo ndani ya shimo la choo.
“Mhhh…. Anatikisa kichwa, Mungu anamiujiza yake….kwa sasa tungekuwa tunaongea mambo mengi kabisa…. Kitu kilichosaidia ni sehemu ya ukuta wa choo chicho chenye matundu manane kutangulia chini kabla ya tundu alimokuwemo kuanguka, hebu fikiria kama tundu alimokuwemo ama matundu hayo ndiyo yangetangulia halafu yangefuatiwa na ukuta wa choo hiki … ingekuwaje angefunikiwa humo…..”alisema kwa majonzi huku akiwa ameinamisha kichwa chake chini. 
Alisema pamoja na miujiza hiyo, kijana hayo hakuweza kufikia uchafu, licha ya kuwa alipata majeraha sehemu mbali mbali za mwili wake huku akilalamikia maumivui sehemu za kifuani , mgongoni na kichwani kidogo.
Hata hivyo, kutokana na ajali hiyo, ambayo ilitokea wakati Mkuu wa shule hiyo akiwa nyumbani kwake nje kidogo na shuleni hapo, alipigiwa simu ambapo walilazimika kumkimbiza mwanafunzi huyo,  katika kituo cha afya cha Mtakatifu Thereza maarufu kama Bugimbi mjini hapa ulioko kama kilometa mbili kutoka shuleni hapo  ambapo alitibiwa na kurudishwa shuleni.
Ilielezwa shuleni hapo kuwa  hili ni tukio la pili la choo cha shule hiyo kutitia shuleni hapo, ambapo choo cha kwanza kilititia mwaka 2009 ikiwa bado inajengwa .
Hata hivyo choo hicho ambacho ni inasemekana kuwa ni cha msaada kilijengwa  mwaka 2010 na kiongozi  mmoja Jumuiya hiyo ya wazazi Mkonia Kagera, katika uchunguzi wa gazeti hili licha ya kutokuwa  na utaalamu wa masuala ya unjenzi ulibani kujengwa chini ya kiwango kwani hata saruji iliotumika ilikuwa ni kiasi kidogo sana ikizingatiwa kuwa eneo hilo la shule ni sehemu ya udongo wa kichanga na ni chepeche (chemichemi) nyakati za mvua  kama kipindi hiki.
Aidha hata nondo  na wavu zilizotumika katika ujenzi  huo, ni wa kiwango cha chini jambo mbalo moja kwa moja yanaweka rehani  roho za watoto  iwapo serikali haitakuwa na tabia ya kukagua hata ubora wa vyoo vinavyotumiwa na wanafunzi shuleni.
Katika shule hiyo ambayo ni mchanganyiko wasichana kwa wavulana kwa sasa  wavulana hawana choo ambapo wanalazimika kutumia choo cha walimu, huku choo cha dharura kilianza kuchimbwa  siku hiyo hiyo ya tukio.
Mwisho.

 Wadau wa UKIWMI katika Manispaa ya Bukoba  na wakiwa katika picha ya pamoja na Mwenyekiti  wa Tume ya Kudhiti Ukimwi Taifa TACAIDS,Dkt. Fatma Mrisho.
 Mkuu wa mkoa wa kwanza wa Kagera , Bw.Samuel Luangisa akisalimia na Mkuu wa Mkoa wa Kagera kwa sasa Kanali Fabian Massawe.
Baadhi ya nyumba wanamoishi wachimbaji wadogo wa madini aina ya dhahabu walioko katika wilaya ya Biharamulo.Kwa kawaida ya nchi ya Tanzania wachimbaji wadogo ndio wamekuwa wa kwanza kuvumbua eneo lenye madini na kisha wawekezaji hujitokeza kutaka kuweka katika eneo hilo na kuanza kufanya utafiti kwa miaka mingi bila serikali kuambulia kitu chochote.


Posted by www.theonestinaj.blogspot.com at 12:03:00 AM No comments:
Email ThisBlogThis!Share to XShare to FacebookShare to Pinterest

Saturday, April 21, 2012

Mawaziri wanne wa JK wadaiwa kuachia ngazi


HATIMAYE mawaziri saba kati ya nane wakiwemo wanaokabiliwa na tuhuma za ubadhirifu,wanadiwa kukubali kuandika barua za kujiuzulu wenyewe kwa kile kilichoelezwa kuwa ni kukinusuru Chama cha Mapinduzi (CCM).
Habari za kuaminika kutoka mjini Dodoma zimesema kuwa mawaziri hao, walilazimishwa kujiuzulu katika kikao cha dharura kilichokuwa chini ya uenyekiti wa Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, kilichofanyika mara tu baada ya kumalizika kwa kikao cha Bunge.
Taarifa zimewataja waliokubali kujiuzulu kuwa ni pamoja na Waziri wa Viwanda na Biashara, Cyril Chami; Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), George Mkuchika; Waziri wa Uchukuzi Omari Nundu; na Waziri wa Afya, Dk. Haji Mponda.
Wengine wanaodaiwa kujiuzulu ni Waziri wa Nishati na Madini, William Ngeleja; Naibu Waziri wa Afya, Lucy Nkya; na Naibu Waziri wa Viwanda, Lazaro Nyarandu.
Hata hivyo, Waziri wa Fedha, Mustafa Mkulo, ambaye alishambuliwa vikali kwa kuitwa kinara wa ufujaji, hakuwepo katika kikao hicho kwa madai kuwa yuko nje ya nchi, anasubiriwa aungane na wenzake kuachia ngazi.
Kujiuzulu kwa mawaziri hao kumekuja baada ya kuzuka kwa mjadala mzito ndani ya Bunge kwa siku mbili mfululizo kuhusiana na tuhuma za ufujaji wa kutisha wa fedha za umma, kiasi cha kusababisha kuwepo kwa azimio la kupiga kura ya kutokuwa na imani na Waziri Mkuu Mizengo Pinda.
Wakati wa majumuisho ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mashirika ya Umma, mwenyekiti wa kamati hiyo, Zitto Kabwe, alilitaka Bunge kuweka ushabiki na itikadi za kisiasa pembeni na kuazimia kwa pamoja kupiga kura za kutokuwa na imani na Pinda kutokana na uzembe wa mawaziri wake.
Kabla ya kujiuzulu huko Spika wa Bunge, Anne Makinda, jana alizima hoja ya kumwajibisha Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, akidai kuwa utaratibu mzima umekiukwa na hivyo hauwezi kufanyiwa kazi katika kikao cha sasa cha Bunge.
Makinda alisema hayo alipokuwa akitoa mwongozo uliyoombwa na Mbunge wa Bumbuli, January Makamba (CCM) kuhusu suala hilo na kudai kuwa wanaoendesha mchakato huo itabidi wasubiri hadi Bunge lijalo.
Makinda ametoa hoja hiyo, wakati idadi kubwa ya wabunge wakiwa wametia saini za kumwajibisha Waziri Mkuu kutokana na ubadhirifu mkubwa unaowahusisha mawaziri watano wa serikali.
Mchakato wa utiaji saini unaosimamiwa na Zitto Kabwe, ulikuwa ukiendelea kwa kasi na habari za kuaminika zinasema kuwa idadi ya walio tayari kuweka saini zao inaweza kufika wabunge 200.
Akuzungumza jana mchana, Zitto alisema kuwa hadi muda huo alikuwa na saini za wabunge 66, huku akidai kuwa wabunge wote wa CUF walikuwa wameandikiwa barua na chama chao kusaini azimio hilo, jambo ambalo litafanya idadi ya wabunge kufikia 80.
Zitto ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya kusimamia Mashirika ya Umma (POAC) alisema kuwa hadi jana majira ya saa 7 mchana, wabunge wa vyama vyote walikuwa wameweka saini azimio hilo isipokuwa wa UDP.
Mawaziri wanaotakiwa kuwajibika ni Waziri wa Fedha, Mustafa Mkulo; Waziri wa Viwanda na Biashara, Cyril Chami na naibu wake, Lazaro Nyalandu; Waziri wa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), George Mkuchika; Waziri wa Nishati na Madini, William Ngeleja; na Waziri wa Uchukuzi, Omar Nundu.
Zitto ambaye pia ni Mbunge wa Kigoma Kaskazini (CHADEMA), alisema wabunge wa CUF 12 wameshasaini azimio hilo na kwamba maagizo yametoka makao makuu ya chama hicho kutaka wabunge wake kusaini kusudio hilo.
Alisema kuwa baadhi ya watu wanasema Waziri Mkuu hana makosa na kwamba anaonewa na kueleza kuwa wanampenda sana, lakini wanaiheshimu zaidi Tanzania.
Alisema kulingana na kanuni za Bunge, wabunge wanaweza kumwajibisha Waziri Mkuu kwa kumpigia kura ya kutokuwa na imani naye.
“Miongoni mwa majukumu ya Waziri Mkuu ni kusimamia shughuli za serikali pamoja na utendaji wa baraza la mawaziri. Mawaziri wameonekana kusimamia wizara zao ambazo zina wizi na ubadhirifu.
“Kuwepo kwa ubadhirifu ni kushindwa kwa Waziri Mkuu kutekeleza majukumu yake…tunajua hawezi kuwawajibisha mawaziri na ndiyo moja ya mambo tunayotakiwa kuyarekebisha kwenye Katiba, lakini yeye tuko naye hapa na sisi ndiyo tuliomthibitisha na tuna uwezo wa kuondoa uthibitisho wake.
“Kwa hiyo katika hilo hatuna mbadala hatuna muafaka kama mawaziri waliotajwa kuhusika na aina ya ubadhirifu kwenye wizara zao, idara zao, mashirika hayo na halmashauri kama hawajachukua hatua tunaanzia na Waziri Mkuu. Atakuwa Waziri Mkuu wa kwanza nchini kupigiwa kura au kutolewa hoja ya kutokuwa na imani naye.
“Tumempa muda mpaka Jumatatu tutawasilisha rasmi hoja yetu kwa Spika kwa mujibu wa mamlaka ya kanuni 133 inayotutaka kukusanya saini ya wabunge asilimia 20 ya wabunge wote ambao kwa hesabu zetu ni wabunge 70 na tutapata zaidi hao,” alisema.
Alisema kwamba wanatimiza matakwa hayo ya kikanuni na kisha kuwasilisha kwa Spika, ili baadaye Bunge liweze kuonyesha meno yake.
Alibainisha kuwa ili Waziri Mkuu aweze kutoka katika kitanzi hicho, anapaswa kumshauri Rais Jakaya Kikwete awafukuze kazi mawaziri hao ama mawaziri hao wajiondoe mapema.
“Lakini kama wanataka kumuweka kiongozi wao, kiraja wao rehani, wanataka Waziri Mkuu aingie katika hoja ya kupigiwa kura ya kutokuwa na imani naye ni jukumu lao, wachague wao wenyewe,” alisema.
Hata hivyo, Spika kwa upande wake alisema kwa mujibu wa kanuni za Bunge ambazo zimetokana na Katiba zinataka hoja kama hiyo iwasilishwe bungeni angalau siku 14 kabla ya siku iliyokusudiwa, na sio wiki ijayo kama ilivyoelezwa juzi na Zitto Kabwe bungeni.
“Sasa hii habari ya kusema waheshimiwa njooni njooni kusaini huo sio utaratibu. Hiyo haikubaliki kwa sababu mimi sijapata hiyo hoja mpaka sasa. Bunge hili tunaahirisha Aprili 23 maanake Jumatatu. Leo (jana), kesho (leo), Jumapili, Jumatatu haikidhi siku 14 sana sana anaweza (Zitto) kukusanya nyaraka labda kuwasilisha Bunge lijalo,” alisema Spika.
Aliendelea kusema kuwa kanuni na utaratibu alioutangaza Zitto hauwezekani na kwamba zoezi la kukusanya saini za wabunge ni batili. Aliwashauri wanaotaka hoja hiyo wavute subira hadi Bunge lijalo, akidai kuwa kuitimiza ndani ya siku tatu zilizobaki ni kukosa mashiko.
Hata hivyo alikiri kuwa wabunge wana madaraka na Waziri Mkuu kulingana na Katiba kwa kuwa ndiyo wanaomwidhinisha baada ya uteuzi.
Alinukuu ibara ya 53(a) (3) kwamba Waziri Mkuu anapitishwa na wabunge ambao wanamthibitisha. “Msingi wa Zitto ni kwamba huyu ni mtu tuliyempitisha sisi wenyewe. Kwa hiyo tuna mamlaka naye kwani ndiye tulimpitisha sisi,” alisema.
“Waziri ndiye atakayekuwa mkuu wa shughuli za serikali bungeni. Serikali chini ya mamlaka ya Rais ndiyo itakayofanya maamuzi juu ya sera. Na mawaziri chini ya uongozi wa Waziri Mkuu watawajibika kwa pamoja katika utekelezaji wa shughuli za serikali. Hivi vifungu ndivyo vinatupa nguvu ya kuwa na uwezo na Waziri MKuu.”
Wabunge wa CCM watishwa
Katika hatua nyingine, imedaiwa kuwa wabunge wa Chama cha Mapinduzi, wameitwa na kutishwa kuchukuliwa hatua ikiwa watasaini azimio hilo.
Mmoja wa wabunge wa CCM aliyekiri kuitwa ni Deo Filikunjombe (Ludewa) ambaye alisema alilazimika kusaini kabla ya kuitikia wito huo.
Filikunjombe, alikiri kuitwa na Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Bunge), William Lukuvi, na kumtaka kutosaini azimio hilo, lakini akamwambia alikwishasaini na alifanya hivyo kwa niaba ya wananchi wa Ludewa ambao wamechukizwa na ubadhirifu mkubwa uliofanywa na watendaji hao wa serikali.
Kuhusu wabunge wa CCM kutosaini azimo hilo, Filikunjombe alisema kanuni haikusema wabunge wote, kwani inafahamika wengine wanarudi nyuma alisema.
Mbunge wa Mtera Livingstone Lusinde alisema suala la hoja ya kikanuni ina lengo la kuchelewesha mchakato wa kuwaondoa wanaolalamikiwa na kuahidi kuwaondoa hata kama Bunge litawakingia kifua.
Alisema kama mawaziri wanaolalamikiwa wataendelea kubakia katika nafasi zao ni bora wabunge wa CCM wakaondoka na kuwaachia wao majukumu yote.
Alipoulizwa kama msimamo wake hauwezi kuwakera viongozi wake na kuamua kumchukulia hatua ikiwa ni pamoja na kumuondoa katika chama, Lusinde alisema kuwa hilo halihofii kwa kuwa hana hati miliki ya ubunge wa Mtera na zaidi ataendelea kubakia Mtanzania anayepigania maslahi ya nchi yake.
Mbunge wa Simanjiro, Christopher ole Sendeka (CCM), alisema katika mapendekezo yaliyoafikiwa juzi hakuna azimio katika kamati yoyote lililotaka waziri aondolewe na kusema kuwa alichokuwa akikifanya Zitto ni usanii.
“Katika taarifa yake ile alipaswa asema Bunge limependekeza mtu fulani awajibishwe, hivyo alitakiwa kuleta nyongeza katika taarifa yake. Hakuna aliyeleta. Ile ni burudani tu,” alisema na kuongeza kuwa hoja hiyo haina mashiko.
Alihoji kuwa iwapo Pinda alishindwa kumuondoa aliyekuwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini, David Jairo, atawezaje kumuondoa Waziri wa Fedha, Mustafa Mkulo.
Alisema kuwa ili hoja hiyo ifanikiwe ni lazima Spika aridhike kwamba ilifuata taratibu na ina sifa hata ikisainiwa na wabunge 200 kama haina sifa haiwezi kupita.
Zitto asema wembe ni uleule
Akizungumzia vikwazo hivyo, Zitto alisema haviwatishi na wanaendelea na mchakato huo, na kwamba watakabidhi hoja hiyo, Jumatatu baada ya kukamilika.
Zitto alisema kama watashindwa kusaini fomu hizo watakuwa wawakilishi wa ajabu kwa kuwa wao ndiyo waliokuwa wakipiga kelele juzi kutaka waliosababisha ubadhirifu kuwajibika na kwamba kama watashindwa kuunga mkono litakuwa ni jukumu la wananchi kupima uwakilishi wao.
Alisema ni jambo la aibu kwa Bunge zima likimaliza kikao bila kuwawajibisha mawaziri waliohujumu mali za taifa.
“Tukiondoka hapa bila kuwawajibisha watu, wananchi huko nje watalidharau Bunge kwa hiyo tunalinda heshima ya Bunge na kulinda heshima ya wabunge kwa kutaka kuona tunaimarisha uwajibikaji.
“Bila watu kuwajibika madudu haya yatarudia na ndiyo maana tunataka uwajibikaji ufanyike,” alisema.
Alisema kuwa anajua wabunge wa CCM wamechukizwa na wizi na ubadhirifu na wamesema kwa nguvu sana juzi na jana na hakuna asiyeona hilo.
“Mimi sijafanya kama mbunge wa CHADEMA, bali kama mbunge wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,” alisema.
Hivyo, alitaka wabunge wasigawanywe katika misingi ya vyama na kwamba anayefanya hivyo hana maslahi na nchi na kuhoji iwapo CCM ina hoja nzuri ambayo inaisimamia.
“Tusiruhusu maneno ya propaganda ya kutugawa na ninyi ndiyo mashahidi mnalalamika na juzi mlimuuliza CAG,” alisema.
Alisema katika masuala ya kitaifa wabunge wanapaswa kuweka pembeni itikadi zao na kuwatumikia wananchi wanaowawakilisha na kusisitiza kuwa wanachokitaka ni mabadiliko na si mapinduzi.
Wasomi waunga mkono
BAADHI ya wananchi wa kada na rika mbalimbali nchini wamesema mwenendo wa Bunge la sasa ni ishara za kuamka kwa mhimili huo inayotokana na changamoto za wabunge wa upinzani.
Wakizungumza na Tanzania Daima kwa nyakati tofauti wananchi hao walisema msimamo wa wenyeviti ambao ni wabunge kutoka upinzani wanaoongoza kamati tatu za Bunge umesaidia kuonyesha uozo wa watendaji serikalini hususan mawaziri wasiotimiza vema wajibu wao.
Wenyeviti wa kamati hizo ni Zitto Kabwe (CHADEMA) Hesabu za Mashirika ya Umma (POAC), Agustine Mrema (TLP) Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) na John Cheyo (UDP) Hesabu za Serikali (PAC).
Kwa mujibu wa Mhadhiri Mwandamizi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) Profesa Issa Shivji, Katiba ya sasa inaruhusu kupiga kura ya kutokua na imani japo ni mapema kufanya hivyo huku akisisitiza kwamba jambo la msingi ni kusubiri uamuzi wa wabunge hao.
Kwa upande wake mhadhiri mwandamizi mstaafu wa UDSM Dk. Azaveli Lwaitama alisema wabunge hao wanagombana na mfumo wa kumweka Waziri Mkuu madarakani hali inayoonyesha wazi kwamba hawana imani na Rais.
“Ninavyoona hapo kinachowachukiza wabunge hao ni uwaziri mkuu na mfumo wa kumpata waziri mkuu kwa sababu wanalalamikia utendaji wa baadhi ya mawaziri lakini waziri mkuu hana uwezo wa kuwafukuza mawaziri hao.
“…Hebu tukumbuke wakati wa Jairo, Waziri Mkuu alitamani kumfukuza akashindwa lakini Katibu Mkuu Kiongozi alikuwa na uwezo; ndiyo maana alimpa likizo yenye malipo.
“Tatizo ni mfumo wa utawala walioteuliwa wanawajibika kwa aliyewateua lakini waliochaguliwa wanatumwa na wananchi ndiyo,” alisema Dk. Lwaitama na kuongeza kwamba lazima mambo hayo yaingie kwenye Katiba mpya.
Mjasiriamali Celina Ezekiel wa Isimani Iringa alisema Bunge limeanza kutambua mamlaka yake ya kuisimamia serikali hasa kwa wabunge wa CCM.
Katibu Mtendaji wa Tume ya Vyuo Vikuu Tanzania (TCU) Profesa Sifuni Mchome alisema wabunge wana uhuru wa kufanya hivyo kwa maslahi ya nchi na kuongeza kwamba ni jambo la kawaida.
Mkazi wa Igunga mkoani Tabora Nicholous Ngassa alisema haafikiani na suala la kumwondoa Waziri Mkuu madarakani badala yake mawaziri walioguswa na ripoti ya CAG wanapaswa kuwajibika na kupelekwa mahakamani.
“Hali ya kutokuwa na imani na Waziri Mkuu na serikali yake kunashusha thamani Chama cha Mapinduzi (CCM) katika jamii na kujiondoa kwenye ramani ya siasa nchini na Afrika,” alisema Ngassa.
Naye Mhadhiri Mwandamizi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam Idara ya Sayansi ya Siasa na Utawala Dk. Benson Bana alisema wabunge wametimiza wajibu wao na kuwataka mawaziri wanaotuhumiwa kuchukua hatua.
Akitolea mfano wa ripoti ya Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) Dk. Bana ambaye ni mwenyekiti mwenza ya Taasisi ya Utafiti wa Elimu ya Demokrasia Tanzania (Redet) alisema umaskini unaongezeka kwa sababu ya wachache walio kwenye ngazi za uamuzi.
“Ripoti ya CAG inaonyesha kushuka kwa kiwango cha uwajibikaji serikalini hususan eneo la matumizi ya fedha za walipa kodi… kwa nini wanaotajwa kwenye ripoti hiyo wasijiuzulu?” alisema Dk. Bana na kutaka wabunge washikamane katika hilo.
Naye Mahadhiri wa Chuo Kikuu cha Kiislam cha Morogoro (MUM) Profesa Juma Mikidadi alisema wabunge wako sahihi katika uamuzi wa kutaka kumjadili Waziri Mkuu kwa sababu ya mawaziri wa chini yake kushindwa kuwajibika.
Sheikh Jabir Ramadhan aliwashauri wabunge hao kutoa muda wa mwisho kwa mawaziri hao ili kabla hawajaondoka waanze kuchunguzwa huku akiwashauri wasifanye hivyo kwa chuki.
Mkazi wa Tabata Jamila Athuman alisema serikali ya awamu ya nne imeongeza pengo kati ya matajiri wachache na maskini wengi hali inayowafanya wananchi kuichukia serikali yao.
“Walioteuliwa hawana uchungu wa nchi ndio maana wanafanya ufisadi huku Rais akiwakingia kifua kwa kuendelea kuwaacha madarakani na wakati mwingine anawahamisha vituo vya kazi,” alisema Jamila.
Joseph Mhimbilila alisema wananchi wamechoka kuvumilia wizi wa mali ya umma unaofanywa na watawala wao sasa wananchi wamechoka hivyo wabunge hao wakishindwa kuwasaidia watachukua hatua kali zaidi.
“Hili linaweza kuwa fundisho kwa viongozi wenye ndoto za kuliibia taifa hili,” alisema.
Kwa Upande wake Mwanasheria Alex Mgongolwa alisema sheria inampa mamlaka Waziri Mkuu kusimamia shughuli zote za serikali na kuhakikisha kunakuwepo na uwajibikaji.
Alisema katika Katiba ibara ya 53 (A 1-6) inasema hoja ya kutokuwa na imani na Waziri Mkuu inaweza kuwasilishwa bungeni kukiwa na sababu za msingi juu ya majukumu ya Waziri Mkuu na kushindwa kuyatekeleza.
“Nafuu inayoweza kupatikana ni kama anayetolewa hoja hajapitisha miezi sita tokea kuteuliwa kwake au kabla ya miezi tisa kupita tokea hoja kama hiyo kuwasilishwa bungeni, na hapa ni lazima Spika ajiridhishe kuwa masharti yamezingatiwa,” alisema Mgongolwa.

source; tanzania daima
Posted by www.theonestinaj.blogspot.com at 4:57:00 AM No comments:
Email ThisBlogThis!Share to XShare to FacebookShare to Pinterest
Newer Posts Older Posts Home
Subscribe to: Posts (Atom)

YALIYOMO

  • ▼  2012 (389)
    • ▼  April (33)
      • "Padri apigwa butwaa kumaliza miaka sita bila kuen...
      • ushirikina mpaka lini?
      • Mwili wa Kanumba unafanyiwa uchunguzi leo
      • kilichomuua Kanumba ni hiki hapa
      • Misa ya mazishi ya Kanumba yanaendelea katika ukum...
      • Jinsi wasanii wenzake walivyokuwa katika msiba huo...
      • RPC Malawi atimuliwa kazi na Rais Banda
      • Haijawahi tokea maziko ya Kanumba labda ya Mwal.Ny...
      • BREKING NEWZZZZZZZ LULU KIZIMBANI CHINI YA ULINZI...
      • ELIZABETH MICHAEL A.K.A LULU KIZIMBANI
      • USAFI UKIWA UMEPAMBA MOTO KATIKA MANISPAA YA BUKO...
      • BILIONI 11 KUJENGA SOKO LA KISASA BUKOBA
      • "KUPATA KIWANJA BUKOBA KWA SASA NI HELA YAKO TU."
      • Katibu Tawala wa Biharamulo ang'olewa jino na JWTZ
      • Bilioni 120 zatumika kuboresha migomba nchini
      • Mawaziri wanne wa JK wadaiwa kuachia ngazi
      • Sijaamini kama nimetoka hai katika ajali hii.
      • Matukio katika picha.
      • "Babu tulikupenda sana, kwa kheri"
      • Upumzike kwa amani Mzee wetu Mpendwa.
      • Elizabeth 'Lulu' apandishwa tena kizimbani, sasa a...
      • Wajumbe wa mkutano Mkuu KCU 1990 Ltd wapigwa mbumb...
      • Tudumishe mila zetu.
      • Ati anamsafirisha Simba kwenye baiskeli!
      • Leo ni siku yangu ya kuzaliwa, asante Mungu kwa ku...
      • Hapo vipi?
      • Mmoja wa wajumbe wa mkutano mkuu wa mezania wa C...
      • 'Hatuondoki, hata kama mkiwaleta kikosi cha FFU'-W...
      • Amani na maendeleo... Kagera, Kagera... Amani na M...
      • Mambo yote ni sawa ilimradi tuvuke salama.
      • Uwepo wa Mungu unapoonekana hivi.......Mugana.
      • Kwa wenzetu wa nchi jirani ya Uganda usalama uko hivi
      • Yaliopita si ndwele, lakini.... Ati wanabeza lugha...
    • ►  May (69)
    • ►  June (120)
    • ►  July (39)
    • ►  August (22)
    • ►  September (15)
    • ►  October (33)
    • ►  November (14)
    • ►  December (44)
  • ►  2013 (118)
    • ►  January (23)
    • ►  February (3)
    • ►  March (2)
    • ►  May (10)
    • ►  June (7)
    • ►  July (22)
    • ►  August (15)
    • ►  September (24)
    • ►  October (3)
    • ►  December (9)
  • ►  2014 (75)
    • ►  January (13)
    • ►  February (7)
    • ►  March (22)
    • ►  April (4)
    • ►  May (5)
    • ►  June (1)
    • ►  July (2)
    • ►  August (6)
    • ►  October (10)
    • ►  November (3)
    • ►  December (2)
  • ►  2015 (13)
    • ►  April (1)
    • ►  May (2)
    • ►  July (10)

KUHUSU MIMI

www.theonestinaj.blogspot.com
BUKOBA, KAGERA, Tanzania
Theonestina Juma, ninaishi Bukoba Kagera Tanzania.Napenda watu wanaojituma kwa kufanya kazi.Sipendi wanaobeza shughuli za wengine.
View my complete profile
Powered By Blogger
Theonestina Juma (Rorya kwetu. Watermark theme. Powered by Blogger.