Wednesday, September 18, 2013

Tanzania, Rwanda na Burundi zasaini mkataba kuzalisha umeme Mto Rusumo



Na Theonestina Juma, Bukoba
TANZANIA, Rwanda na Burundi zimesaini mkataba wa makubaliano ya awali ya kuanza utekelezaji wa mradi wa kufufua umeme katika maporomoko ya mto Rusumo  ya megawati 80.
Mkataba wa makubaliano hayo yamesainiwa  jana (leo) katika Manispaa ya Bukoba ambapo ulihudhuriwa na  wajumbe  mbali mbali kutoka nchi zote tatu.
Akifungua mkutano wa kusaini makubaliano  ya mradi huo, Waziri wa Nishati na Madini nchini, profesa Sospeter Muhongo alisema hatua hiyo inafungua mlango wa kuanza utekelezaji wa mradi huo.
Alisema mradi huo unatarajiwa kuanza mwaka 2015 hadi 2018 ambapo utakuwa takribani miaka minne hadi kukamilika kwake.
Alisema katika utekelezaji wa mradi huo umegawanyika katika sehemu mbili ambapo sehemu ya kwanza wataanza kufufua nishati hiyo, ambayo itagharimu  dola milioni 340 kwa pande za nchi zote tatu na itafadhiliwa na Benki ya Dunia  baada ya kuonesha nia.
Halikadhalika sehemu nyingine ni ujenzi wa njia ya kusafirishia nishati hiyo kutoka mto Rusumo hadi Nyakanazi  katika njia ya kwenda nchi jirani ya Burundi, itakagharimu dola milioni 130.
Alisema kati ya hizo fedha ndizo zitajumuisha masuala ya kufidia watu ambao watatakiwa kuondoka katika maeneo yao kupisha utekezaji wa mradi huo, ambapo  Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB)imeshaonesha nia ya kutoa  dola milioni 95.
Halikadhalika kati ya dola hizo milioni 130 benki zingine nazo zimekubali katika kuwasaidia, ambapo alizitaja benki hizo kuwa ni pamoja na Beenki ya misaada ya ujerumani ( KFW), benki ya ujasiliamali ya ujerumani na benki ya Uholanzi.
Profesa Muhongo alisema pindi mradi huo utakapokamilika  utaweza kuzalisha umeme megawati 80 ambapo kila nchi itapata mgawao sawa ambao ni megawati 27.
Hata hivyo,Waziri Muhongo alitoa tahadhari kwa pande zote za nchi hizo tatu kuwa makini katika harakati za utekelezaji wa mradi huo, kwa kuondoa ukiritimba unaoweza kujitokeza na kusababisha kuvunjika kama ilivyotokea kwa Jumuiya ya Afrika Mashariki mwaka 1977.
“Katika harakati za utekelezaji wa mradi huu, lazima nchi zote kuwa makini, kuondoa ukiritimba unaoweza kujitokeza ya mtu kuajiri ndugu zake… hasa masuala ya rushwa…,tunahitaji umeme kwa ajili ya maendeleo ya wananchi”alisema.
Alisema iwapo mradi huo utakamilika nchi zote tatu zitaweza kuwa na nishati hiyo ya kutosha na hata kuanza kujenga mtandao kwa nchi jirani kwa lengo la kuwauzia.
Alisema hadi kufika mwaka 2015 Tanzania itakuwa na megawati ya umeme 3,000 ambapo kwa sasa  nchi unao megawati 1,501.2.
Naye Waziri wa Miundombinu kutoka nchini Rwanda, Profesa Silas Rwakabamba akizungumza katika mkutano huo, kabla na baada ya kusaini mktaba wa makubaliano hayo, alisema mradi huo utakapokamilika utawezesha wananchi kupata umeme wa kutosha na hivyo kuwa kichocheo cha ukuwaji wa uchumi katika nchi hiyo.
“Mimi ni shahidi katika makubaliano haya kwa nchi yangu, tunaamini nishati ya umeme ni muhimu katika ukuaji wa uchumi na maendeleo ya wananchi”alisema.
Mradi wa kufufua umeme katika  maporomko ya mto Rusumo  kupendezwa kuanza  tangu mwaka 1974 , ambapo hata hivyo utekelezaji wake haukuweza kuendelea hadi mwaka 2005 upembuzi yakinifu ulipoanza na kwa sasa utekelezaji wake unaanza.
Mawaziri waliohudhuria katika mkutano huo ni pamoja na Profesa Sospeter Muhongo kutoka Tanzania, Waziri wa Miundombinu, Profesa Silas Rwakabamba  wa Rwanda na  Waziri wa nishati na Madini, Bw. Manirakiza C'ome kutoka nchini  Burundi na Naibu Kamishna wa nishati ya masuala ya umeme nchini, Mhandisi Innocent Luoga.
 Pia wawakilishi kutoka benki ya Maendeleo ya  Afrika, Bi. Stella Mandago na wa Benki ya Dunia, Bw. Paul Baringanire.

No comments:

Post a Comment