Friday, September 6, 2013

CCM Muleba watwangana makonde mkutanoni



Na Theonestina Juma, Muleba
KATIKA hali isiyo ya kawaida baadhi ya wajumbe wa Kamati kuu ya Halmashauri kuu ya  CCM wilaya ya Muleba nusura watwangane makonde ukumbini wakigombania sababu ya CCM kumwongezea muda  aliyekuwa katibu wa CCM wilayani, Bw. Wilbroad Msafiri baada ya kustaafu kwa mujibu wa kanuni.
Tukio hilo la aina yake ambayo lilikuwa kama kichekesho kwa wajumbe hao limetokea  jana (leo) wilayani humo, baada ya wajumbe hao kutofautiliana ukumbini hapo, huku kukiwa na kundi la wajumbe wachache waliokuwa wakiunga mkono kurejeshwa huku asilimia kubwa wakipinga.
Hatua hiyo ilikuja muda mchache kabla ya wajumbe hao kumkataa Katibu huyo kwa kupiga kura za ndiyo au hapana.
Mkutano huo maalum uliokuwa na agenda moja tu kulingana na maelezo ya Mwenyekiti wa CCM Wilaya, Bw. Muhaji Bushako  kilikuwa ni kumpokea Katibu wao au kumkataa na ulihudhuriwa na wajumbe wapatao 151 kutoka katika kata zote za wilaya ya uleba ambapo kura tano tu ndizo zilimkubali Katibu huyo kuendelea huku kura 146 zikimkataa.
Hata hivyo, kabla ya kufikia hatua ya kupiga kura ukumbuni humo kulikuwa hakukaliki, ambapo Kamanda wa vijana CCM wilaya ya Mleba, Bw. Mushuti aliamuru vijana wake kuwatoa nje kwa nguvu baasdhi ya wajumbe waliokuwa wakirushiana maneno makali, karibia watwangane makonde.
Hata hivyo, baadhi ya wajumbe wa mkutano huo maalum wakizungumza  kwa nyakati tofauti walisema kuwa sababu ya kumkataa Katibu huyo ni kutokana na kutokuwa na ushirikiano na baadhi ya wachama wilayani humo na pia ni mfitini.
Bw. Evad Ernest alisema kamati ya siasa ilikaa tarehe tofauti mwezi jana baada ya kupata fununu kuwa Katibu huyo ameongezewa  mkataba wa mwaka mmoja na sekretariet ya kamati kuu ya CCM  Taifa kuendelea kukaa Muleba jambo ambalo walipiga kwani walimtaka apelekwe katika wilaya nyingine.
Alisema sababu ya kumkataa ni kutokana na kutokuwa na ushirikiano  baina ya wanachama, pia anatumia vibaya fedha za Chama
“Tunashangaa huyu mtu anaongezewa muda tena anakuja Muleba, wakati alishatuaga kuwa amestaafu na anarudi kwao kupumzika mambo ya siasa, sasa iweje tena aletwe Muleba… sisi hatumtaki apelekwe wilaya nyingine”alisema
“Muda wote aliokaa Muleba hakuna na ushirikiano na  viongozi wenzake, ni mtu mwenye fitina ana eneza majungu kwa baadhi ya viongozi wenzake,ni mbinafsi amekigawa chama katika makundi, hali iliofanya CCm kuendelea kushindwa katika chaguzi mbali mbali wilayani hapa”aliongeza.
Alitoa mfano kuwa katika uchaguzi wa mwaka 2010 Katibu wao ndiye alikuwa chanzo cha CCM kupoteza kata 12 na kwenda upinzani baada ya kujitwisha madaraka  ambapo aliondoa baadhi ya wagombea walioshinda kura za maoni na kuwaweka watu wake.
Naye Mwenyekiti wa CCM, Wilaya ya Muleba Bw. Bushako aliwazuia wajumbe hao kuacha kufunga ofisi ya Katibu kama ambavyo baadhi ya wajumbe walivyopendekeza na badala yake aliwataka wafuate utaratibu na kanuni ya Chama.
Alisema mambo yanayofuata watalazimika kuyapeleka katika vikao vya ngazi ya juu ya CCM ambapo waliwataka kila mtu kuheshimu mawazo ya watu wachache bila kuathiri kanuni za Chama hicho.
“Kulingana na kanuni za Chama sisis hatuna malmaka ya kumfungia ofisi ya Katibu na badala yake mamlaka yetu yanafikia hapa ya kumkataa kwa kupiga kura”alisema Mwenyekiti huyo.
Hata hivyo kutokana na maelezo yake hayo, wajumbe hao walianza  kumzomea ambapo wao walitaka ofisi hiyo ifungwe mara moja na wala asiingie humo tena.
Hata hivyo gazeti hili lilipompigia simu, Bw. Msafiri ili kuweza kusikiliza upande wake baada ya kukataliwa na wajumbe hao simu yake ilipokelewa na mwanamke ambaye hakutaka kuzungumza na baadaye kukata simu.
Mwisho.

No comments:

Post a Comment