Saturday, September 14, 2013

Baadhi ya wanawake Rorya wadaiwa kuwatishia kuwaua waume zao wanaopinga uvuvi haramu



Na Theonestina  Juma, Rorya
KUNDI la wavuvi  wapatao 168 wakiwa na boti 21 wamewatia kiwewe wavuvi wadogo  wa mwalo wa Busanga, Kata ya Nyamtinga wilayani Rorya kwa kuhofia samaki kuisha, baada ya kuvamia hifadhi ya samaki ya Mang’ereng’ere katika Ziwa Victoria na kuanza kuvua samaki wakitumia, sumu na makokoro yaliyo chini ya milimita saba na urefu wa mita 120.
Kundi hilo la wavuvi  hao imeelezwa kuwa walifika katika mwalo wa Busanga mwishoni mwa mwezi wa Julai, ambapo makokoro hayo hunasa kila aina samaki ikiwemo na mayai hali inayowatia wasiwasi wavuvi wadogo kuisha kwa samaki mwalo huo katika eneo hilo.
Wavuvi hao wanadaiwa kutimuliwa kila mwalo walikofika katika ziwa Victoria upande wa mkoa wa Mara kutokana na aina ya zana wanazozitumia mfano kama mwalo wa kinesi na mto mara, kutokana na kuharibu mazalia ya samaki ambapo huvua hadi mayai na samaki wachanga.
Wavuvi hao wanadaiwa kuharibu hifadhi za samaki za mang’ereng’ere  kata ya Nyamtinga na Nyabiwe kata ya kirogo maeneo ambayo yametengwa na serikali kwa ajili ya mazalia ya samaki.
Wakizungumza na gazeti hili baadhi ya wavuvi kutoka katika mwao huo, walisema kundi hilo la wavuvi kutoka maeneo ya Kibui Kata ya Nyamunga kutokana kuendesha shughuli zao za uvuvi kwa zana zisizoruhusiwa, wamekuwa wakifanya shughuli hiyo bila kutumia taa za kama inavyopaswa na badala yake hutumia mwanga wa tochi tu.
“Hawa wavuvi  wanavua samaki wengi mno,kwa siku hupata  samaki kama madebe 30-50,wachanga, wakati na wakubwa, hali inayowafanya kusafirisha kwenda kuuza nchini Kenya na wengine huwapeleka Musoma na Tarime”alisema mvuvi mmoja.
Wavuvi hao walisema si kwamba wanawaonea gele, bali hofu  kwa baadhi ya walaji wa bidhaa hiyo kwani kuna wengine wanawavua kwa kutumia sumu na pia kutoweka kabisa kwa samaki  aina zote za  samaki katika hifadhi hiyo na eneo hilo kutokana na kuharibu mazalia ya samaki.
Halikadhalika walisema kundi hilo la wavuvi wanaojiita ‘By sisi ‘ wamekuwa wakiwatambia kuwa hakuna anayeweza kuwachukulia hatua wala kuwazuia kwa sababu wanafahamiana na viongozi wote na Busanga ndiko kwao.
Kutokana na tambo hizo, baadhi ya wanawake  wa kijiji hicho, ambao ni wachuuzi wa samaki, wametishia  kuwauwa baadhi ya wanaume kwa kuwawekea sumu kwenye chakula kwa  watakaosababisha wavuvi hao kutimuliwa kijijini hapo.
“Tunapokuambia taarifa hii, hatutaki hata majina yetu yafahamike, kwani hata baadhi ya wanawake wa kijiji hiki hatutaki wasikie tunazungumza kuhusu nini, kwa sababau  imefikia hatua ya kututishia maisha kama tutathubutu hawa watu wazuieliwe kuvua samaki kwa mfumo huu ama kufukuzwa katika eneo hili”alisema mmoja wao kwa sauti ya chini mno.
Walisema samaki wanaovua ni pamoja na Nembe, Gogogo, Mumi,Sangara, Furu, Ningu, Sato na dagaa, ambapo wao hakuna aina ya samaki wanaolenga.   
Hata hivyo, wavuvi hao walionesha kutikishwa na uongozi wa kijiji hicho kuitisha mkutano wa kijiji ghafla na kuondoa wasimamizi wa mwalo huo kwa madai kuwa wanakula fedha , ambapo hayo yote yalitokana na baada ya wavuvi hao kuwasili kijiji hapo,na walikuwa wakipingwa mfumo wa uvuvi wao na BMU.
Hata hivyo upande wa mwenyekiti wa kijiji cha Busanga, Bw. Paul  Festo  hakuweza kupatikana kupitia simu yake ya mkononi kila alipopigiwa na gazeti hili.
Aidha  Afisa wa Doria katika ziwa Victoria mkoa wa Mara, Bw. Meela akizungumza na gazeti hili kwa njia ya simu , alisema malalamiko hayo ameshayapokea katika ofisi yake kutoka kwa raia mwema ambapo anayashughulikia.
“Taarifa hizo nimezipokea, nitakujulisha baada ya kuwasiliana na afisa uvuvi wa Wilaya ya Rorya, na baadaye nitakueleza ni hatua gani tulizozichukua”.
Hata hivyo, hadi mwandishi wa habari anatuma habari hizi, tayari Afisa doria, Bw. Meela ameshawasili wiayani Rorya katika mwalo huo, na kushudia hali halisi, huku akikosa ushirikiano kutoka kwa wavuvi wa kijiji hicho, ambapo kundi hilo linadaiwa kupata taarifa mapema ya ujio wa afisa huyo na kufanikiwa kuficha makokoro yao, ambapo wamebahatika kupata za wavuvi wa eneo hilo ambao nao wanaendesha uvuvi haramu.
Hali hiyo imethibitishwa na Bw. Meela ambapo  wakazi wa eneo hilo wanashindwa kutoa ushirikiano kwao, ambapo tayari watu hao walishaficha nyavu zao na ameahidi kuzitafuta hadi zipatikane.
Habari zaidi zinasema kuwa Afisa huyo ameshuhudia samaki waliovuliwa  hadi mayai na kundi hilo na wavuvi wanaotumia zana haramu ambapo amewataka kuondoka eneo hilo mara moja na kuacha kuendesha uvuvi  usiostahili katika eneo hilo.

No comments:

Post a Comment