Sunday, September 15, 2013

Ndani ya siku 10 Operesheni Kimbunga, yanasa wahamiaji haramu 6,809 na ng'ombe 2,809



Na Theonestina Juma,Bukoba
OPERESHENI kimbunga inayoendeshwa kwa kushirikisha vyombo vyote vya usalama katika mikoa ya Kagera, Kigoma na Geita ya kuwarejesha wahamiaji haramu makwao na  kuwasaka majambazi wanaotumia silaha imewezesha kuwakamata wahamiaji haramu  6,809 na  watuhumiwa wa ujambazi 32.
Hayo yamebainishwa leo na Naibu Kamisheni wa Operesheni Kimbunga,Simon Sirro ambaye pia ni Mkuu wa Operesheni nchini wakati akizungumza na waandishi wa habari mjini Bukoba .
Kamanda Sirro alisema jumla ya wahamiaji haramu 6,809 waliokamatwa, Wanyarwanda ni 1,446, Warundi 4,229, Waganda 647, Wakongo 443, wasomali 42, Yemen mmoja na India pia mmoja na kwamba watu hao wamekamatwa katika mikoa yote mitatu.
Alisema kati ya hao wahamiaji haramu 2,367 wamerejeshwa makwao kwa maamuzi ya mahakama, 1,866 wamerudi nchini mwao kwa hiari ,396 wameachiwa huru huku wengine 2,170 wanaendelea kuhojiwa.

 Mabomu sita risasi 265 zilizokamatwa
Watuhumiwa wa ujambazi 32 wa unyang'anyo wa  wanaotumia silaha wamekamatwa ambapo wote wamebainika ni raia wa Tanzania baada ya kukimbiwa na wenzao kutoka nchi jirani wanaoshirikiana nao katika kufanya uhalifu ambapo Kagera wamekamatwa majambazi 20, Geita watano na Kigoma saba.
Kamanda Sirro alisema pamoja na majambazi kutoka nchi jirani kuondoka baada ya kupewa wiki mbili, lakini anaamini kuwa watarejea tena na hivyo  kuwataka kuwachana na kazi hiyo kwani hailipi.
“Biashara ya ujambazi hailipi, na tunaamini kuwa watarejea tu, kuendelea kutumia silaha zao, tunawambia  hata nasi tunatumia silaha tena ndiyo kalamu zetu za kila siku, hivyo waachane na kazi hiyo watafute kazi nyingine”alisema.
Halikadhalika risasi 265 za bunduki aina ya  SMG/SAR zimekamatwa  huku za Mark iv 20 zikipatikana na 82 zikiwa ni za magobole ambapo pia  imekamatwa mitambo miwili ya kutengeneza magobole pamoja na sare za jeshi la nchi jirani.
Kamanda Sirro alisema katika operesheni hiyo,wamefanikiwa kukamata mabomu sita ya kutupwa kwa mikono na silaha 22 za aina mbali mbali za moto  zilizokuwa zikitumika katika uhalifu.
Kuhusu mifungo, ng’ombe 2,809 nao wamekamatwa ambapo katika mkoa wa Kigoma wamekamatwa 559, Geita wamepatikana 95 na Kagera ni 2,155, jambo ambalo Kamanda Sirro ameoneshwa kusitikishwa kutokana na mapori yote yamejaa mazizi ya ng’ombe na hivyo kufanya hata wanyama waliomo katika mapori hayo kutoishi kwa amani.
Upande wa baadhi ya wahamiaji haramu kulalamika kuwa wananyanyaswa hasa na Maafisa Uhamiaji, Kamanda Sirro alisema kuwa hakuna mhamiaji haramu anayenyanyaswa kama baadhi yao wanavyodai, kwani zoezi hilo linazingatia sheria, kanuni, utaratibu zilizopo na haki za binadamu.

No comments:

Post a Comment