Monday, September 16, 2013

Mnyarwanda mwingine ajinyonga ni katika Operesheni kimbunga, kisa hakutaka kurudi kwao

Na Theonestina Juma, Kagera,

RAIA mwingine wa Rwanda, Bw.Michael John (70) amejinyonga kwa kutumia shuka lake chumbani kwake Wilayani Missenyi,akihofia kurejeshwa nchini Rwanda na Operesheni kimbunga inayoendelea.

Akizungumza na gazeti hili Mtendaji wa kijiji cha Lwano, Bw.Deusdedith NjunwaMulokozi alisema tukio hilo limetokea usiku wa kuamukia  leo Septemba 16,mwaka huu, katika kitongoji cha Chaibumba kijiji cha Lwano kata ya Ishozi Tarafa  ya Kiziba Wilayani Missenyi.

Alisema Bw.John  alikutwa na mkewe Bi.Rahel Kagawa (66), mwili wake ukiwa unaning’inia juu ya dari akiwa tayari ameshakata roho saa 1.07 asubuhi baada ya usiku kukorofishana na mumewe huyo na kuamua kwenda kulala kwa jirani.

Alisema chanzo cha Bw. John kujinyonga ni baada ya kupata taarifa kuwa wahamiaji haramu wote wanarejeshwa nchini mwao, ambapo toka siku hiyo alikuwa akisema kuwa hawezi kurudi Rwanda na badala yake atajiua.

“Chanzo cha Bw. John kujiua ni kuhofia kurejeshwa nchini mwake Rwanda, ambapo alikuwa akikataa kurudi huko kwa madai kuwa alitoka huko akiwa kijana na hawezi kurejea tena nchini humo”alisema mtendaji huyo.

Alisema Bw. John  aliingia  kijijini hapo tangu mwaka 1983 hadi leo hadi mauti yanamkuta, ambapo alioa mwanamke wa Kitanzania  Bi. Rahel ambaye ni mzaliwa wa kijiji cha Ishozi  na kuishi naye kwa kipindi cha miaka 30 na hawakufanikiwa kupata mtoto.

Alisema kabla ya kuchukua hatua hiyo, Bw. John alikuwa akikorofishana na mkewe  na kukimbia kwenda kulala kwa majirani kutokana na ulevi na kurudi kesho yake asubuhi na kumkuta akiwa katika hali nzuri.

“Kwa siku ya jana mkewe aliamua kukimbia na kwenda kulala kwa majirani kama ilivyo kwa wanadoa wanapokorofishana na alirejea asubuhi ili kuweza kuangalia kama hali imetulia kutokana na ulevi, lakini matokeo yake amemkutaka akiwa ameshajinyonga”alisema.

Alisema  Bi. Rahel aliporejea nyumbani alikuta mlango ukiwa umefungwa ambapo si kawaida yake,  alilazimika kutumia nguvu kufungua mlango huo na kukuta mumewe akiwa amejinyonga.

Alisema wanandoa hao walikuwa wakiishi maisha ya kawaida tu na walikuwa wakijishughulisha na kazi ya kilimo pekee.

Mtendaji huyo ametoa wito kwa wahamiaji haramu walioko katika kijiji hicho kuacha tabia ya kujiua kwani sio jibu na badala yake  wafuate sheria na utaratibu unaotakiwa na serikali kama wanapenda kuishi nchini.
Hili ni tukio la pili la wahamiaji  haramu kujingonga, baada ya, Bw. Francis Mathias (75),mkazi wa kitongoji Kikukuru kata Kikukuru, tarafa Mabira wilayani kujinyonga Septemba 9, mwaka huu baada ya mkewe kugoma kuuzwa mali zote ili warejee nchini Rwanda

No comments:

Post a Comment